Rais Samia Suluhu

  • Mheshimiwa Rais Samia atoa mwelekeo mchakato wa katiba mpya

    Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amesema anatambua umuhimu wa katiba mpya kama ambavyo maoni ya makundi mbalimbali, ikiwemo kikosi kazi, yaliyotolewa na kusisitiza kuendelezwa kwa mchakato huo ambao ulikwama tangu mwaka 2014. Licha wa umuhimu huo ametahadhari kuwa upatikanaji wa katiba mpya ni mchakato na kwamba mchakato huo sio mali ya wanasiasa bali ni ya Watanzania wote, hivyo amewataka wanasiasa kutokuhodhi sauti kwenye mchakato huu. “Katiba ni ya Watanzania, awe ana chama, awe hana, awe ana dini, awe hana, awe mrefu, awe mfupi, mnene, mwembamba, mkubwa, mdogo. Kwa hiyo matengenezo yake yanahitaji tafakuri kubwa sana,” amesema Mheshimiwa Rais. Hata hivyo, amesema kuwa katiba si kitabu, bali ni misingi ya maadili, itikadi na namna ambavyo Watanzania wanakubaliana kuendesha Taifa lao, hivyo, makubaliano hayo yanaandikwa, hivyo, haiwezi kuwa sawa na nchi nyingine. “Tunaanza na elimu Watanzania wajue [katiba] ni kitu gani […] Kwa hiyo tusiwaburuze wananchi. Katiba viongozi wa kisiasa si mali yetu, ni mali ya Watanzania. Tunachokitaka kwenu ni maoni katiba iweje,” ameongeza. Aidha, ameongeza demokrasia lazima iakisi namna watu ndani ya nchi yanavyoendesha masuala yao ikiwemo tamaduni, maadili, mila, desturi, na kwamba huwezi kuchukua demokrasia kutoka nchi nyingine na kuiingiza nchini bila kuzingatia masuala ya ndani. Read More

  • Mageuzi ya Mheshimiwa Rais yanayoongeza ufanisi wa mashirika ya umma

    Katika kutelekeza maelekezo ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kuhakikisha kuwa mashirika na taasisi nyingine za Serikali au zile ambazo Serikali ina hisa nyingi zinajiendesha kwa faida, Msajili wa Hazina, Nehemia Mchechua ameainisha hatua tano za kimkakati ambazo zitachochea mabadiliko katika ufanisi wa taasisi hizo. Kwanza amesema ni kujenga utamaduni wa kukutana katika kikao kazi kila mwaka na watendaji na wenyeviti wa taasisi hizo. Pili, ni mabadiliko ya sheria ambayo yatahusisha kuondoa sheria zilizopitwa na wakati au zinazokwamisha mashirika kujiendesha kwa ufanisi. Hatua ya tatu ni kuangalia namna ya kuwapata viongozi wa kuendesha taasisi hizo ili kuhakikisha kuwa wanaopewa dhamana ni wenye ujuzi stahiki ambapo Mheshimiwa Rais amewahi kupendekeza kuwa nafasi hizo ziwe zinatangazwa, ili watu wenye sifa watume maombi. Nne ni uboresha wa bodi za taasisi hizo kwa kuangalia namna zinavyoteuliwa ambapo amesema lengo ni kuchagua watu wenye uwezo wa kiutendaji na kukabiliana na changamoto zinazojitokeza. Hatua ya tano ni kutoa uhuru kwa taasisi hizo kuajiri ambapo mchakato huo tayari umeanza na kwa hatua ya kwanza wanaanza na taasisi za kibiashara na vyuo vikuu. Mchechu amesema baada ya hatua hizi, hatua zaidi za kimabadiliko zitachukuliwa ndani ya taasisi moja moja na viongozi husika na kuwa lengo ni kuziwezesha kuwa na ufanisi, kuongeza faida na kutoa gawio serikalini ili kupunguza utegemezi wa ruzuku. Read More

  • Madaktari Wamarekani walioalikwa na Rais kufanya upasuaji bure

    Madaktari bingwa 60 wa mifupa na nyonga kutoka Los Angeles, Marekani wanatarajiwa kuwasili nchi Agosti 10 mwaka huu kwa ajili ya kutoa huduma za matibabu bure ya upasuaji wa magoti na nyonga katika Hospitali ya Rufaa ya Seliani inayomilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT). Madaktari hao wanakuja kwa mwaliko wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na watawasili nchini kupitia Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa Kilimanjaro (KIA) ambapo wanatarajiwa kufanya upasuaji kwa wagonjwa 200 kwa wiki mbili ambapo walengwa ni wananchi wenye hali ya chini. Kuja kwa madaktari hao ni fursa kwa wananchi wenye changamoto hizo kupata msaada ambapo pengine wasingeweza kumudu gharama hizo kwani gharama za upasuaji huo ni kubwa ambazo hufika hadi TZS milioni 75, lakini zitatolewa bure na wataalamu hao. Mbali na kutoa huduma hiyo, madaktari hao pia watatoa mafunzo kwa madaktari bingwa wa hospitali hiyo kuhusu upasuaji wa magoti, mifupa na nyonga, ili hata watakapoondoka, huduma hizo ziendelee kutolewa kwa viwango vya juu zaidi. Ili kuwezesha hilo, Serikali sikivu chini ya Mheshimiwa Rais imeruhusu vifaa vitakavyotumika kwenye upasuaji, dawa na vitendea kazi vingine viingizwe nchini bila kulipiwa kodi. Read More

  • Uwazi Serikalini: Soma na pakua hapa muhtasari wa ripoti ya Tume ya Haki Jinai

    Read More

  • Mheshimiwa Rais abadili miundo ya wizara ili kuchochea ufanisi na maendeleo

    Kufuatia kutungwa kwa Sheria ya Mipango ya Taifa ya Mwaka 2023 pamoja na uamuzi wa kuhamishia masuala ya uwekezaji Ofisi ya Rais, hivyo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amefanya mabadiliko madogo ya miundo ya wizara na kufanya uteuzi wa viongozi. Mheshimiwa Rais ameunda Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji ambapo amemteua Prof. Kitila Mkumbo kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji. Prof. Mkumbo ni mbunge wa jimbo la Ubungo. Pili, ameunda Wizara ya Fedha ambapo amemteua Dkt. Mwigulu Nchemba kuwa Waziri wa Fedha. Kabla ya uteuzi huo Dkt. Nchemba alikuwa Waziri wa Fedha na Mipango. Pia, ameunda Wizara ya Viwanda na Biashara ambapo amemteua Dkt. Ashatu Kijaji kuwa Waziri wa wizara hiyo. Kabla ya uteuzi huo Dkt. Kijaji alikuwa Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara. Amemteua Lawrence Mafuru kuwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango ya Taifa. Kabla ya uteuzi huu Mafuru alikuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha na Mipango (Usimamizi wa Uchumi). Mwisho, amemteua Elijah Mwandumbya kuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha (Usimamizi wa Uchumi). Kabla ya uteuzi huo Mwandumbya alikuwa Kamishna, Idara ya Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha na Mipango. Read More

  • USAID yampongeza Rais Samia kwa mageuzi ya kiuchumi na kisiasa

    Mageuzi ya kiuchumi, kisiasa na kijamii anayoendelea kuyafanya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa manufaa ya Watanzania wote yameendelea kuwavutia wengi wanaopongeza juhudi zake ambapo mwisho wa wiki Msimamizi wa Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Marekani (USAID), Bi. Samantha Power ametoa pongezi zake kwa Rais kwa juhudi zake katika kuendeleza mageuzi ya kidemokrasia na ushirikishwaji wa wananchi. Bi. Power amesema kuwa jitahda za Rais Samia zimewezesha Tanzania kupanua ushirikiano wa kimaendeleo na kuifanya iwe rahisi kwa sekta binafsi ya Marekani kuizingatia Tanzania kama mahali pazuri pa kuwekeza. Aidha, ameeleza kuwa kazi ya kuvutia uwekezaji na biashara itakuwa rahisi Tanzania ikiendelea na mageuzi katika maeneo ya utawala na kusisitiza kuwa makubaliano ya malengo ya maendeleo yanatoa fursa ya kuongeza mara mbili zaidi mafanikio yaliyopatikana katika ushirikiano imara kati ya nchi hizo mbili. Amempongeza Rais pia kwa ushirikishwaji wa wananchi, hususani vijana, katika shughuli za maendeleo akisema tofauti na maeneo mengine ambayo vijana huchukuliwa kama Taifa la kesho, kwa Tanzania vijana ndio Taifa la sasa. Kupitia ujenzi wa uchumi shirikishi kwa kutumia teknolojia ameeleza imani yake kuwa Tanzania itanufaika kwani wananchi wake wengi ni vijana. Pongezi zaidi amezitoa kwa Rais kwa namna Tanzania inavyotumia teknolojia kupitia Programu ya M-Mama inayowawezesha wajawazito kupata huduma zinazowawezesha kuokoa maisha yao, hasa katika maeneo ya vijijini ambapo hadi sasa imepunguza vifo vya uzazi kwa asilimia 38. Read More

  • Kila halmashauri kunufaika na ajira mpya zaidi ya 8,000 kwenye sekta ya afya

    Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan anaendelea kutekeleza ahadi ya kutoa ajira ili kuongeza ufanisi Serikali ambapo sasa zimetangazwa nafasi za ajira 8,070 katika kada ya afya ambazo mchakato wake unakaribia kukamilika muda wowote kuanzia sasa. Ajira hizo zitawezesha Serikali kupeleka watoa huduma kwenye halmashauri zote nchini, uhitaji ambao umeendelea kuongezeka kutokana na kasi kubwa ya Rais Samia kujenga na kuboresha vituo vya kutolea huduma za afya. Huu ni mwendelezo wa Rais kutoa ajira kwenye kada hiyo ambapo kwa mwaka 2021/22 alitoa ajira kwa watumishi afya 7,736. Mbali na ajira hizo mpya katika sekta ya afya, Aprili mwaka huu Serikali pia ilitangaza kutoa ajira 13,130 za ualimu wa shule za msingi na sekondari, uhitaji ambao nao umeongezeka kutokana na ujenzi wa shule na madarasa pamoja na kuongezeka kwa wanafunzi. Ajira hizi mbali na kuboresha huduma kwa mamilioni ya Watanzania, pia zitawawezesha wote watakaoajira kuboresha maisha yao pamoja na ya wategemezi wao, hatua ambayo itapunguza changamoto za ajira nchini. Read More

  • Bandari ya Dar es Salaam yaipita Bandari ya Mombasa kwa ufanisi

    Bandari ya Dar es Salaam imeendelea kuwa na mchango muhimu katika ukuaji wa uchumi, ajira, mapato ya serikali na ukuzaji wa sekta nyingine. Uwezo wake wa kuhudumia mizigo umeendelea kuimarika ambapo makasha yaliyohudumiwa yameongezeka kufikia makasha 63,529 mwaka 2022 kutoka makasha 56,198 mwaka 2021. Ripoti ya Benki ya Dunia (The Container Port Performance Index 2022) imeiweka Bandari ya Dar es Salaam katika nafasi ya kwanza kwa ufanisi Afrika Mashariki ikiipita Bandari ya Mombasa nchini Kenya kutoka na kuimarika kwa ufanisi ambao umepunguza kwa muda ambao meli zinatumia bandarini, jambo ambalo ni muhimu kwa kukuza ushindani wa kibiashara. Katika ripoti hiyo ya dunia imeiweka Bandari ya Dar es Salaam katika nafasi ya 312, huku Mombasa ikiwa nafasi ya 326. Dar es Salaam imepanda kwa nafasi 49 ikitoka nafasi ya 361 mwaka 2021, huku Mombasa ikishuka kwa nafasi 30 kutoka 296 mwaka 2021. Mafanikio hayo ni matokeo ya uwekezaji wa takribani bilioni 1 uliofanyika bandarini ukihusisha upanuzi wa gati namba 1 hadi 7 kwa kuongeza kina kutoka mita 7 hadi mita 14.7 ambazo zinaruhusu meli kubwa yenye uwezo wa kubeba mizigo tani 6,500 kutia nanga. Maboresho mengine ni mashine za kisasa za kupakua mizigo ambazo zinafanyakazi kwa kasi mara mbili ya awali mikakati ambayo sambamba na uimiarisha matumizi ya TEHAMA imeongeza mara mbili idadi ya meli za mizigo zilizokuwa zikihudumiwa bandarini. Aidha, ikilinganishwa na nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), bandari ya Dar es Salaam imepanda kwa nafasi tatu kutoka nafasi ya 9 mwaka 2021 hadi nafasi ya 6 mwaka 2022. Ukuaji huu umeendelea kuwa na matokeo chanya katika kuvutia uwekezaji na biashara, ajira zaidi na kuongeza mapato ya Serikali yanayorudi kuwahudumia Watanzania. Read More

  • ZAMA MPYA: Diaspora sasa kushiriki shughuli za kiuchumi na kijamii kidijitali

    Mchango wa Watanzania waishio nje ya nchi na wale wenye asili ya Tanzania katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi umeendelea kukua mwaka hadi mwaka ambapo kwa mwaka 2022 waliwekeza nchini TZS bilioni 2.5 kupitia Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja. Aidha, takwimu za Benki ya Kuu ya Tanzania (BoT) zinaonesha kuwa Diaspora ambao hadi sasa ni milioni 1.5, mwaka 2021 walituma nchini TZS trilioni 1.3, huku kiwango hicho kikiongezeka mara mbili mwaka 2022 kufikia TZS trilioni 2.6. Kutokana na nafasi yao hii jalili katika ustawi wa jamii na maendeleo, Serikali imeandaa mfumo wa kidijitali wa kuwasajili Diaspora wenye asili ya Tanzania (Diaspora Digital Hub) utakaoiwezesha kupata taarifa zao na wao kupata taarifa muhimu kutoka nchini. Mfumo huo wa aina yake utawezesha Serikali kupata taarifa sahihi za Diaspora kama vile jinsia, elimu na utaalamu na kuwawezesha Diaspora kushiriki kidijitali katika shughuli mbalimbali za maendeleo ambapo wataweza kupata huduma za kibenki, hifadhi ya jamii, fursa za uwekezaji, biashara na masoko, masuala ya uhamiaji, vitambulisho vya taifa na huduma nyingine ambazo watazifikia kiurahisi. Diaspora wamekuwa wakichangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi kupitia biashara ya mali zisizohamishika (real estate) ambapo mwaka 2021 walinunua nyumba na viwanja vyenye thamani ya TZS bilioni 2.3 huku mwaka 2022 ununuzi huo ukipanda hadi TZS bilioni 4.4. Read More

  • Tanzania ya pili Afrika matumizi ya TEHAMA kuhudumia wananchi

    Tanzania imetajwa na Benki ya Dunia (WB) kuwa nchi ya 26 duniani na ya pili barani Afrika kwa kuwa na mfumo madhubuti wa matumizi ya Teknolojia ya Mawasiliano na Habari (TEHAMA) katika kutoa huduma kwa wananchi, utaratibu ambao unawezesha huduma kupatikana kwa wakati na unafuu. Katika utafiti huo wa GovTech Maturity Index (GTMI) 2022 uliofanywa na Benki ya Dunia na kuhusisha nchi 198 umeiweka Tanzania katika Kundi A ikipanda kutoka Kundi B mwaka 2021 ambapo kwa dunia ilikuwa nafasi ya 90 na Afrika nafasi ya tano, ambapo matumizi ya TEHAMA yamekuwa kwa asilimia 0.86 kwa mwaka uliopita. Tanzania imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuimarisha matumizi ya teknolojia ya kidijitali kwenye kutoa huduma kwa umma, ambapo hivi karibuni Rais Samia Suluhu Hassan alishuhudia utiaji saini mikataba ambayo itakwenda kufikisha huduma ya mawasiliano kwa Watanzania zaidi ya milioni 8, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati huo. Utafiti huo umeonesha kuwa sekta za elimu, afya, huduma za fedha kwa simu na kilimo ndizo sekta zinazoongoza kutoa huduma kwa umma kwa kutumia TEHAMA. Mkakati huo umeendelea kufanikiwa kutokana na hatua za Serikali kuweka mazingira rafiki na kuwainua wabunifu wa kidijitali. Kufikishwa kwa mawasiliano kwenye vijiji ambavyo havikuwa na huduma hiyo hapo awali kutapanua zaidi wigo wa Watanzania wanaoweza kunufaika na huduma za kidijitali za Serikali, na hivyo kukuza kiwango cha Tanzania kwa upande wa Afrika na dunia katika tafiti zijazo. Read More