May 2023

  • Kila halmashauri kunufaika na ajira mpya zaidi ya 8,000 kwenye sekta ya afya

    Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan anaendelea kutekeleza ahadi ya kutoa ajira ili kuongeza ufanisi Serikali ambapo sasa zimetangazwa nafasi za ajira 8,070 katika kada ya afya ambazo mchakato wake unakaribia kukamilika muda wowote kuanzia sasa. Ajira hizo zitawezesha Serikali kupeleka watoa huduma kwenye halmashauri zote nchini, uhitaji ambao umeendelea kuongezeka kutokana na kasi kubwa ya Rais Samia kujenga na kuboresha vituo vya kutolea huduma za afya. Huu ni mwendelezo wa Rais kutoa ajira kwenye kada hiyo ambapo kwa mwaka 2021/22 alitoa ajira kwa watumishi afya 7,736. Mbali na ajira hizo mpya katika sekta ya afya, Aprili mwaka huu Serikali pia ilitangaza kutoa ajira 13,130 za ualimu wa shule za msingi na sekondari, uhitaji ambao nao umeongezeka kutokana na ujenzi wa shule na madarasa pamoja na kuongezeka kwa wanafunzi. Ajira hizi mbali na kuboresha huduma kwa mamilioni ya Watanzania, pia zitawawezesha wote watakaoajira kuboresha maisha yao pamoja na ya wategemezi wao, hatua ambayo itapunguza changamoto za ajira nchini. Read More

  • Nafasi za ajira mpya 520 kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)

    Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan anaendelea kuongeza nafasi za ajira katika taasisi mbalimbali za Serikali ili kuboresha utoaji huduma kwa wananchi. Read More

  • Bandari ya Dar es Salaam yaipita Bandari ya Mombasa kwa ufanisi

    Bandari ya Dar es Salaam imeendelea kuwa na mchango muhimu katika ukuaji wa uchumi, ajira, mapato ya serikali na ukuzaji wa sekta nyingine. Uwezo wake wa kuhudumia mizigo umeendelea kuimarika ambapo makasha yaliyohudumiwa yameongezeka kufikia makasha 63,529 mwaka 2022 kutoka makasha 56,198 mwaka 2021. Ripoti ya Benki ya Dunia (The Container Port Performance Index 2022) imeiweka Bandari ya Dar es Salaam katika nafasi ya kwanza kwa ufanisi Afrika Mashariki ikiipita Bandari ya Mombasa nchini Kenya kutoka na kuimarika kwa ufanisi ambao umepunguza kwa muda ambao meli zinatumia bandarini, jambo ambalo ni muhimu kwa kukuza ushindani wa kibiashara. Katika ripoti hiyo ya dunia imeiweka Bandari ya Dar es Salaam katika nafasi ya 312, huku Mombasa ikiwa nafasi ya 326. Dar es Salaam imepanda kwa nafasi 49 ikitoka nafasi ya 361 mwaka 2021, huku Mombasa ikishuka kwa nafasi 30 kutoka 296 mwaka 2021. Mafanikio hayo ni matokeo ya uwekezaji wa takribani bilioni 1 uliofanyika bandarini ukihusisha upanuzi wa gati namba 1 hadi 7 kwa kuongeza kina kutoka mita 7 hadi mita 14.7 ambazo zinaruhusu meli kubwa yenye uwezo wa kubeba mizigo tani 6,500 kutia nanga. Maboresho mengine ni mashine za kisasa za kupakua mizigo ambazo zinafanyakazi kwa kasi mara mbili ya awali mikakati ambayo sambamba na uimiarisha matumizi ya TEHAMA imeongeza mara mbili idadi ya meli za mizigo zilizokuwa zikihudumiwa bandarini. Aidha, ikilinganishwa na nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), bandari ya Dar es Salaam imepanda kwa nafasi tatu kutoka nafasi ya 9 mwaka 2021 hadi nafasi ya 6 mwaka 2022. Ukuaji huu umeendelea kuwa na matokeo chanya katika kuvutia uwekezaji na biashara, ajira zaidi na kuongeza mapato ya Serikali yanayorudi kuwahudumia Watanzania. Read More

  • ZAMA MPYA: Diaspora sasa kushiriki shughuli za kiuchumi na kijamii kidijitali

    Mchango wa Watanzania waishio nje ya nchi na wale wenye asili ya Tanzania katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi umeendelea kukua mwaka hadi mwaka ambapo kwa mwaka 2022 waliwekeza nchini TZS bilioni 2.5 kupitia Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja. Aidha, takwimu za Benki ya Kuu ya Tanzania (BoT) zinaonesha kuwa Diaspora ambao hadi sasa ni milioni 1.5, mwaka 2021 walituma nchini TZS trilioni 1.3, huku kiwango hicho kikiongezeka mara mbili mwaka 2022 kufikia TZS trilioni 2.6. Kutokana na nafasi yao hii jalili katika ustawi wa jamii na maendeleo, Serikali imeandaa mfumo wa kidijitali wa kuwasajili Diaspora wenye asili ya Tanzania (Diaspora Digital Hub) utakaoiwezesha kupata taarifa zao na wao kupata taarifa muhimu kutoka nchini. Mfumo huo wa aina yake utawezesha Serikali kupata taarifa sahihi za Diaspora kama vile jinsia, elimu na utaalamu na kuwawezesha Diaspora kushiriki kidijitali katika shughuli mbalimbali za maendeleo ambapo wataweza kupata huduma za kibenki, hifadhi ya jamii, fursa za uwekezaji, biashara na masoko, masuala ya uhamiaji, vitambulisho vya taifa na huduma nyingine ambazo watazifikia kiurahisi. Diaspora wamekuwa wakichangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi kupitia biashara ya mali zisizohamishika (real estate) ambapo mwaka 2021 walinunua nyumba na viwanja vyenye thamani ya TZS bilioni 2.3 huku mwaka 2022 ununuzi huo ukipanda hadi TZS bilioni 4.4. Read More

  • Mradi wa gesi asilia Lindi kutoa ajira za moja kwa moja 8,000

    Fursa za Watanzania kuendelea kunufaika na rasilimali zao zinaendelea kuongezeka ambapo awamu hii ni mradi kusindika gesi asilimia mkoani Lindi ambao unatajiwa kutoa ajira zaidi ya 8,000 kwa Watanzania pamoja na kuongeza matumizi ya nishati salama majumbani na maeneo mengine, kukuza uchumi na kuchochea ukuaji wa sekta nyingine. Baada ya majadiliano yaliyodumu kwa takribani miaka miwili Tanzania na kampuni za uchimbaji wa mafuta na gesi za Equinor, Shell pamoja na Exxon Mobil zimefikia makubaliano kwa ajili ya uchimbaji wa gesi asilia, mradi ambao utagharimu zaidi ya TZS trilioni 70. Kupitia mradi huo ambao ujenzi wake unatarajiwa kuanza Juni 2025 mbali na ajira hizo za moja kwa moja, Watanzania zaidi watanufaika kwa ajira zisizo za moja kwa moja kwa kutoa huduma za kifedha, chakula na malazi, usafiri na usafirishaji, ulinzi, afya na mawasiliano. Aidha, kuhakikisha Watanzania wananufaika na uwekezaji huo mikataba yote inayoingiwa itapitiwa na kuidhinishwa na Baraza la Mawaziri kama ambavyo Sheria ya Petroli ya mwaka 2015 ambapo mikataba mitano iliyoingiwa ikipitishwa na baraza itasainiwa Juni 2023. Mradi huo utaongeza mapato ya Serikali, Shirika la Maendeleo Tanzania (TPDC) litapata gawio kubwa, pia Watanzania watajengewa uwezo katika sekta ya gesi ikihusisha pia uhamilishaji teknolojia. Read More

  • Tanzania ya pili Afrika matumizi ya TEHAMA kuhudumia wananchi

    Tanzania imetajwa na Benki ya Dunia (WB) kuwa nchi ya 26 duniani na ya pili barani Afrika kwa kuwa na mfumo madhubuti wa matumizi ya Teknolojia ya Mawasiliano na Habari (TEHAMA) katika kutoa huduma kwa wananchi, utaratibu ambao unawezesha huduma kupatikana kwa wakati na unafuu. Katika utafiti huo wa GovTech Maturity Index (GTMI) 2022 uliofanywa na Benki ya Dunia na kuhusisha nchi 198 umeiweka Tanzania katika Kundi A ikipanda kutoka Kundi B mwaka 2021 ambapo kwa dunia ilikuwa nafasi ya 90 na Afrika nafasi ya tano, ambapo matumizi ya TEHAMA yamekuwa kwa asilimia 0.86 kwa mwaka uliopita. Tanzania imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuimarisha matumizi ya teknolojia ya kidijitali kwenye kutoa huduma kwa umma, ambapo hivi karibuni Rais Samia Suluhu Hassan alishuhudia utiaji saini mikataba ambayo itakwenda kufikisha huduma ya mawasiliano kwa Watanzania zaidi ya milioni 8, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati huo. Utafiti huo umeonesha kuwa sekta za elimu, afya, huduma za fedha kwa simu na kilimo ndizo sekta zinazoongoza kutoa huduma kwa umma kwa kutumia TEHAMA. Mkakati huo umeendelea kufanikiwa kutokana na hatua za Serikali kuweka mazingira rafiki na kuwainua wabunifu wa kidijitali. Kufikishwa kwa mawasiliano kwenye vijiji ambavyo havikuwa na huduma hiyo hapo awali kutapanua zaidi wigo wa Watanzania wanaoweza kunufaika na huduma za kidijitali za Serikali, na hivyo kukuza kiwango cha Tanzania kwa upande wa Afrika na dunia katika tafiti zijazo. Read More

  • Kazi ya Rais Samia kuimarisha TEHAMA inavyoboresha maisha ya kila Mtanzania

    Dunia ikiendelea kushika kasi katika matumizi ya kompyuta kwenye mambo mbalimbali, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan hajaiacha Tanzania nyuma kwani anatekeleza ahadi yake ya kukuza sekta ya teknolojia, habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili vijana wengi zaidi waweze kujiajiri, lakini pia kurahisisha na kuboresha utoaji huduma kwa wananchi. Mei 13 mwaka huu aliongoza utiaji saini miradi miwili ya ujenzi wa minara 758 katika Kata 713 pamoja na mradi wa kuongeza uwezo wa minara 304 ya mawasiliano hatua ambayo itafikisha mawasiliano na huduma ya intaneti kwa Watanzania zaidi ya milioni nane waishio vijijini, maeneo ambayo awali hayakuwa na huduma hizo. Ili kuwezesha wananchi kunufaika na uwepo wa miundombinu hiyo, Rais Samia ameweka wazi dhamira ya Serikali anayoiongoza kupunguza gharama za intaneti kwa kuanza na kupunguza gharama za uendeshaji kampuni za mawasiliano, hatua ambayo itawezesha kampuni hizo kupunguza gharama za vifurushi, hivyo wananchi wengi, mathali waliojiajiri kupitia TEHAMA, waweza kumudu gharama. Asema kuwa Serikali inalifanyia kazi suala la gharama kubwa za kupitia mkongo kwa Taifa kwenye hifadhi ya barabara na pia Serikali itafikisha umeme kwenye minara ya mawasiliano ili kupunguza gharama za uendeleshaji mnara mmoja kutoka TZS shilingi milioni 1.8 kwa mwezi hadi TZS 400,000, hatua ambazo zitapunguza gharama za vifurushi. Rais Samia anachukua hatua hizi akiamini kuwa uwepo wa mawasiliano bora na intaneti nchi nzima kutachochea ukuaji wa sekta nyingine kama afya, elimu, kilimo, uchumi, haki pamoja na ulinzi na usalama kwani wananchi wataweza kupata taarifa sahihi kwa wakati, watapata njia ya kutoa maoni yao pamoja na kuimarika kwa biashara na uchumi wa kidijitali. Ni wazi pia kuwa, kwa hatua hizi za Rais Samia anaweka mazingira wezeshi ya kuanzisha viwanda vya uzalishaji wa vifaa vya TEHAMA vyenye uwezo wa kutoa ajira kwa wananchi wengi, kudhibiti majanga na kuchochea tafiti katika sekta mbalimbali. Read More

  • Utayari wa kisiasa wa Rais Samia utakavyoipa Tanzania katiba bora

    Uamuzi wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan wa kufufua mchakato wa kuipata Katiba Mpya uliokwama tangu mwaka 2014 umeonesha utayari wa kisiasa wa ofisi hiyo ya juu zaidi nchini kuleta Mabadiliko (Reformation) kama alivyoeleza kwenye msingi wa 4R za uongozi wake. Aidha, kurejeshwa mezani kwa mchakato huo kumethibitisha pamoja na mambo mengine kuwa Rais Samia ni msikivu, na anafanyia kazi maoni anayopokea kwa pendekezo la kufufua mchakato huo lilitolewa na kikosi kazi alichokiunda mwaka jana kwa ajili ya kutathmini hali ya kisiasa nchini. Kama wasemavyo Wahenga kuwa Ukimulika Nyoka Anzia Miguuni Pako, ndivyo Rais alivyofanya kwani Kamati Kuu ya CCM, chama anachokiuongoza, Juni 2022 iliielekeza Serikali kuangalia namna ya kufufua mchakato huo ambapo sasa TZS bilioni 9 zimetengwa kwa ajili ya shughuli hiyo. Utayari wake wa kisiasa umeweza kuufikisha mchakato hadi ulipo sasa ambapo mwanga unaonekana kuelekea kulifikia lengo, huku wadau mbalimbali wakimpongeza kwa kuvuka vikwazo vyote ndani ya Serikali na chama chake kwani amewahi kusema yeye mwenyewe kuwa uamuzi huo si kila mmoja anakubaliana nao. Amepongezwa pia kwa namna anavyoufanya mchakato huo kuwa shirikishi ukihusisha majadiliano ya vyama vyote, wanadau na wananchi kwa ujumla akiamkini kuwa maboresho yanayokwenda kufanyika ni kwa ajili ya manufaa ya Watanzania, hivyo ni lazima washirikishwe. Read More

  • Muda wa kulipa nyumba Magomeni Kota: Badala ya miaka 15, sasa ni miaka 30

    Wakazi 644 wa Magomeni Kota mkoani Dar es Salaam waligoma kusaini mkataba wa kuanza kununua nyumba za eneo hilo kwa madai kwamba bei pamoja na muda wa malipo uliopangwa haukuwa rafiki kwao na wala hauendani na hali zao za kiuchumi ambapo walipaza sauti zao kumuomba Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kuingilia kati suala hilo. Mwenyekiti wa Wakazi hao wa Magomeni Kota, George Abel alisema bei za nyumba hizo ni kubwa, zisizoendana na uwezo wao, hivyo hawawezi kuimudu licha ya Serikali kuzishusha bei ikilinganishwa na hali ya soko. Wakazi hao walipaza sauti wakimuomba Rais Samia kuongezewa muda wa kulipia nyumba hizo kutoka miaka 15 iliyokuwepo awali hadi miaka 30 hali ambayo itapunguza kwa asilimia 100 kiasi ambacho wananchi hao wanapaswa kulipa kila mwezi. Rais Samia Suluhu Hassan, aliye msikivu na anayejali wananchi wote, alipokea maombi hayo na ameyafanyia kazi na sasa wananchi wa Magomeni Kota watalipa nyumba zao kwa kipindi cha miaka 30 kama walivyoomba, muda ambao wakazi wote wa eneo hilo wamekiri kuwa ni rafiki na kila mmoja amekiri ataweza kukamilisha malipo yaliyopunguzwa Ikumbukwe pia Machi 23, 2021, wakati Rais Samia akizindua nyumba hizo aliitaka TBA kupunguza gharama za uuzaji wa nyumba hizo kwani zipo juu kwa wananchi wa kawaida, hivyo pamoja na kupunguzwa bei pia sasa wananchi watalipa nyumba hizo kwa muda mrefu zaidi “Pamoja na kuwa kipato chetu kimekuwa kidogo kwa sababu ya kustaafu lakini, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kupata unafuu wa nyongeza hii ya muda, kwa sasa naamini sote tunaweza kujitahidi kukamilisha jambo hili (malipo),” alisema Ramadhan Mkenze mkazi wa Magomeni Kota. Read More

  • Rais anayejali: Sasa vipimo vya awali kwa wajawazito kutolewa bure

    Serikali imetangaza kuwa huduma za vipimo vya awali kwa wajawazito ambazo zinahusisha kupima wingi wa damu, mkojo ili kuangalia wingi wa protini, shinikizo la damu pamoja na kusikiliza mapigo ya moyo ya mtoto, zitatolewa bure. Kutolewa bure kwa vipimo hivyo muhimu kutawawezesha wajawazito kujua mwenendo wa ujauzito, kuepuka kifafa cha mimba na vifo vya mama na mtoto ambapo lengo la Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2021/22-2025/26) ni kupunguza vifo vya uzazi kutoka vifo 321 kwa vizazi 100,000, hadi vifo 220 na vifo vya watoto kutoka vifo 51 kwa vizazi hai 1,000 hadi vifo 40. Aidha, hatua hii itaongeza zaidi idadi ya wajawazito wanaohudhuria kliniki pamoja na kujifungulia kwenye vituo vya afya ambapo Serikali imeahidi itahakikisha upatikanaji wa 100% wa dawa za kuzuia kutoka damu wakati wa kujifungua, dawa za kuongeza damu na dawa za kuzuia kifafa cha mimba katika vituo vyote afya vya umma. Hatua hizi ni mwendelezo wa kazi kubwa aliyofanya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu wa kujenga vituo vya afya, kuboresha miundombinu ya afya nchi nzima, kuajiri maelfu ya watumishi wa afya pamoja na kununua vifaa tiba, hivyo kuiarisha huduma za afya vijijini ambapo awali hali ilikuwa ngumu zaidi. Imani juu ya huduma za afya zinazoendelea kutolewa kwenye vituo vya afya imeendelea kuongezeka kwani kwa mujibu wa Utafiti wa Demografia na Afya mwaka 2022, idadi ya wajawazito waliotembelea kliniki walau mara nne kati ya wajawazito 100 imeongezeka kutoka 53 mwaka 2015/16 hadi 65 mwaka 201/22 kati huku wanaojifungua chini ya uangalizi wa mtoa huduma mwenye ujuzi ikiongezeka kutoka 66 hadi 85 katika kipindi hicho. Read More