Kila halmashauri kunufaika na ajira mpya zaidi ya 8,000 kwenye sekta ya afya

Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan anaendelea kutekeleza ahadi ya kutoa ajira ili kuongeza ufanisi Serikali ambapo sasa zimetangazwa nafasi za ajira 8,070 katika kada ya afya ambazo mchakato wake unakaribia kukamilika muda wowote kuanzia sasa.

Ajira hizo zitawezesha Serikali kupeleka watoa huduma kwenye halmashauri zote nchini, uhitaji ambao umeendelea kuongezeka kutokana na kasi kubwa ya Rais Samia kujenga na kuboresha vituo vya kutolea huduma za afya.

Huu ni mwendelezo wa Rais kutoa ajira kwenye kada hiyo ambapo kwa mwaka 2021/22 alitoa ajira kwa watumishi afya 7,736.

Mbali na ajira hizo mpya katika sekta ya afya, Aprili mwaka huu Serikali pia ilitangaza kutoa ajira 13,130 za ualimu wa shule za msingi na sekondari, uhitaji ambao nao umeongezeka kutokana na ujenzi wa shule na madarasa pamoja na kuongezeka kwa wanafunzi.

Ajira hizi mbali na kuboresha huduma kwa mamilioni ya Watanzania, pia zitawawezesha wote watakaoajira kuboresha maisha yao pamoja na ya wategemezi wao, hatua ambayo itapunguza changamoto za ajira nchini.