July 2023

  • Tanzania ni ya mfano Afrika kwa uwekezaji katika rasilimali watu

    Wakuu wa nchi za Afrika, viongozi wa ngazi mbalimbali na wadau wengine wamekusanyika Tanzania kujadili mustakabali wa rasilimali watu barani Afrika ambapo Rais wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu ametumia jukwaa hilo kueleza hatua mbalimbali ambazo Tanzania imezichukua kuimarisha sekta hiyo ambayo ni pamoja na kutenga fedha kwa ajili ya afua mbalimbali za lishe na huduma za afya ya uzazi wa mama na mtoto. Hatua nyingine ni kuimarisha upatikanaji wa huduma za afya na elimu ili kuondoa udumavu ambao, mara nyingi, hupunguza kiwango cha uelewa na uwezo wa kusoma kwa waoto na kuhakikisha watoto wanaandaliwa kimwili, kiakili, kiisimu/kijinsia kiubunifu na kiakili-hisia. Aidha, Serikali imetoa afua kwa kaya masikini, inatoa elimu bila malipo kuanzia ngazi ya awali hadi kidato cha sita, inapanua elimu ya ufundi na mafunzo ya amali, imefuta ada kwa baadhi ya vyuo vya ufundi, imeanza kutoa mikopo kwa vyuo vya kati, inatoa mikopo kwa vijana, inaruhusu waliokatisha masomo kurejea shule pamoja na kuweka mkakati wa kuvutia vijana kwenye kilimo, yote haya yakilenga kuongeza mchango wao kwenye uchumi. Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi mwaka 2022, vijana ndio kundi lenye watu wengi zaidi nchini Tanzania, hivyo hatua ambazo Rais ameeleza kuwa Tanzania imezichukua kwa asilimia kubwa zimewalenga vijana kwani anaamini kwamba maisha bora ambayo vijana wengi hukimbilia Ulaya kuyafuata yanaweza kupatikana barani Afrika endapo Serikali zao zitawawezesha. “Viongozi wenye maono hujenga sera zao kwenye maendeleo ya watu na kufuatiwa na maendeleo ya vitu,” amesema Rais Samia akitoa wito kwa viongozi wenzake wa Afrika na kusisitiza kwamba Afrika haitoweza kuendelea endapo rasilimali watu isipoendelezwa. Read More

  • Isome hapa hotuba ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu katika Mkutano wa Rasilimali Watu Afrika

    Read More

  • Mikakati ya Rais Samia unavyoweka rekodi ya uwekezaji Tanzania

    Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kimesajili miradi ya uwekezaji 229 yenye thamani ya TZS trilioni 4.5 kati ya Januari hadi Juni mwaka huu, ambapo lengo ni kufikia miradi 400 ifikapo Desemba 2023. Idadi hiyo inadhihirisha kasi kubwa ya usajili wa miradi nchini ikilinganishwa na miradi 293 iliyosajiliwa mwaka 2022, hivyo kusajili asilimia 78 ya miradi hiyo ndani ya nusu mwaka ni mafanikio makubwa kwa nchi. Kusajiliwa kwa miradi hiyo inayotoa ajira zaidi ya 30,000 kwa Watanzania katika sekta mbalimbali ni matokeo ya sera ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini, ikiwemo kuboresha sheria, kupunguza tozo/kodi mbalimbali na kuimarisha amani na utulivu. Aidha, takwimu zinaonesha mkakati huo wa Rais umefanikiwa zaidi kwani kwa miaka sita ya Serikali ya awamu ya tano, jumla ya miradi ya TZS trilioni 45 ilisajiliwa, huku miaka miwili ya Serikali ya awamu ya sita ikisajili miradi ya trilioni 22 ndani ya miaka miwili, takwimu zinazoonesha kuwa itafanya vizuri kuliko awamu iliyopita. Aidha, sababu nyingine ni taasisi 12 za usimamizi kuwa katika jengo moja hivyo kurahisisha utoaji huduma pamoja na matumizi ya TEHAMA yaliyorahisisha utoaji wa leseni na vibali mbalimbali vya biashara na uwekezaji hasa kupitia dirisha ya kielektroniki ambapo mwekezaji sasa anaweza kuwasilisha maombi akiwa popote dunia Read More

  • Uwazi Serikalini: Soma na pakua hapa muhtasari wa ripoti ya Tume ya Haki Jinai

    Read More

  • Rais Samia aitaka Tanzania kuchangamkia fursa zinazojitokeza

    Kwa mara ya kwanza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amezungumza hadharani kuhusu suala la uwekezaji na uendeshaji wa Bandari ya Dar es Salaam kwa kushirikiana na sekta binafsi akisisitiza kuwa ni mihimu kama nchi tukatumia fursa zinazojitokeza kabla hazijaondoka au kukwapuliwa na washindani wetu, wakati tukibaki kulumbana. Ametoa rai hiyo Ikulu jijini Dar es Salaam alipokuwa akiwaapisha viongozi aliowateua karibuni, mmoja wao akiwa ni Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo na kumueleza kwamba moja ya majukumu yake ni kuangalia changamoto na fursa zilizopo nchini ili zitumike vizuri kwa manufaa ya Watanzania. “Wakati sisi tunalumbana, bandari apewe nani, iende, isiende, wenzetu kwa kuona malumbano yetu wame-jump [kimbilia] wamekwenda kule kule […] sasa muone jinsi fursa zinavyokuja na kukimbia haraka haraka, na jinsi wengine wanavyoweza kuzitumia haraka haraka,” amesema. Amesema kazi kubwa iliyopo nchini ni kuleta mabadiliko, lakini kwenye nia safi ya kujenga nchi mabadiliko yanakaribishwa na kwamba licha ya kuwa watu hawajazoea, kwa kwenda nao taratibu na kadiri watakavyoendelea kuona matokeo, watazoea. Kupitia uwekezaji unaokusudiwa bandarini, Tanzania inalenga kuongeza uwezo wa bandari kufadhili bajeti ya nchi kw asilimia 30, kuzalisha ajira zaidi ya 70,000, kuongeza mapato ya Serikali, kupunguza muda wa kuhudumia meli, kuongeza uwezo wa bandari kupokea meli kubwa na kuifanya bandari hiyo kukidhi viwango vya kimataifa. Read More

  • Mama Yuko Kazini, Ajira zinazidi kuongezeka

    Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan anaendelea kuongeza nafasi za ajira katika taasisi mbalimbali za Serikali ili kuboresha utoaji huduma kwa wananchi. Read More

  • Tanzania yavunja rekodi ya uwekezaji ya miaka 10

    Mei mwaka huu Tanzania ilivunja rekodi iliyodumu kwa miaka 10 kwa kusajili miradi mpya ya uwekezaji 52 yenye thamani ya TZS bilioni 783, ikitarajiwa kuzalisha ajira zaidi ya 6,200 ikiwa ni matokeo ya sera za kibiashara za Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Tangu alipoingia madarakani Machi 2021, Rais Samia ameifungua nchi na kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini hatua ambayo imerejesha imani ya wawekezaji ambao wameiona Tanzania ni sehemu salama ya kuwekeza mabilioni yao ya mitaji pamoja na kuvutia uwekezaji mpya. Kutokana na mkakati huo mwamko wa wakezaji wa ndani nao umekuwa mkubwa kuchangamkia fursa zinazojitokeza ambapo kwa mujibu wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) asilimia 50 iliyosajiliwa kati ya Aprili hadi Juni mwaka huu inamilikiwa na wazawa, mingine ikiwa ni ya wageni na ubia, ikiwa ni ongezeko kutoka asilimia 20 iliyokuwepo Januari. Ongezeko la uwekezaji nchini limeendelea kuwa na manufaa kwa Watanzania ambapo zaidi ya ajira za moja kwa moja 30,000 zinatokana na miradi yote iliyosajiliwa kati ya Januari hadi Juni mwaka huu, huku kukiwa na maelfu ya fursa za ajira zisizo za moja kwa moja. Manufaa mengine ni kuchochea ukuaji wa uchumi, pia kuongezeka kwa uwekezaji kunajenga imani kwa wawekezaji wapya kuja nchini. Katika kurahisisha biashara na uwekezaji, Serikali imeanzisha kituo cha pamoja ambacho kina jumla ya taasisi 12 zinazohusika na sekta hiyo ambacho kinarahisisha utoaji wa leseni, vibali na nyaraka nyingine muhimu ndani ya muda mfupi. Aidha, Mei mwaka huu TIC imeanza kutumia mfumo wa Dirisha la Pamoja la Kuhudumia Wawekezaji la Kielektroniki Tanzania (TeIW) ambalo limekuwa suluhisho katika kurahisha upokeaji wa maombi, utoaji wa huduma za vibali, leseni na usajili kwa wawekezaji kwa haraka. Lengo la Mfumo huo ni kutumika kurahisisha mtiririko wa taarifa kati ya taasisi zote zilizoko ndani ya kituo. Read More

  • Mheshimiwa Rais abadili miundo ya wizara ili kuchochea ufanisi na maendeleo

    Kufuatia kutungwa kwa Sheria ya Mipango ya Taifa ya Mwaka 2023 pamoja na uamuzi wa kuhamishia masuala ya uwekezaji Ofisi ya Rais, hivyo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amefanya mabadiliko madogo ya miundo ya wizara na kufanya uteuzi wa viongozi. Mheshimiwa Rais ameunda Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji ambapo amemteua Prof. Kitila Mkumbo kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji. Prof. Mkumbo ni mbunge wa jimbo la Ubungo. Pili, ameunda Wizara ya Fedha ambapo amemteua Dkt. Mwigulu Nchemba kuwa Waziri wa Fedha. Kabla ya uteuzi huo Dkt. Nchemba alikuwa Waziri wa Fedha na Mipango. Pia, ameunda Wizara ya Viwanda na Biashara ambapo amemteua Dkt. Ashatu Kijaji kuwa Waziri wa wizara hiyo. Kabla ya uteuzi huo Dkt. Kijaji alikuwa Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara. Amemteua Lawrence Mafuru kuwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango ya Taifa. Kabla ya uteuzi huu Mafuru alikuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha na Mipango (Usimamizi wa Uchumi). Mwisho, amemteua Elijah Mwandumbya kuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha (Usimamizi wa Uchumi). Kabla ya uteuzi huo Mwandumbya alikuwa Kamishna, Idara ya Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha na Mipango. Read More

  • Rais Samia apongezwa kwa kufuta tozo ya kutuma fedha

    Watumiaji wa huduma za kifedha kwa simu wenye akaunti zaidi ya milioni 44 wamefurahia hatua ya serikali ya kuondoa tozo ya kutumia fedha, hatua ambayo imeanza kutekelezwa na kampuni za mawasiliano ya simu kuanzia Julai Mosi mwaka huu ili kuondoa utozaji tozo mara mbili kwenye muamala mmoja. Utekelezaji huo ni matokeo ya Serikali chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kuifanyia marekebisho Sheria ya Mifumo ya Malipo ya Taifa, Sura ya 437 ambapo lengo ni kuchochea ufanyaji wa miamala kwa njia za kielektroniki ili kukuza uchumi wa kidijiti (cashless economy). Watoa huduma za mawasiliano na wananchi waliotoa maoni yao kuhusu uamuzi huo wamesema kuondolewa kwa tozo za Serikali kumepunguza gharama ya kutuma fedha, hatua itakaypchochea ongezeko la miamala kwa njia ya simu, hasa kwa kufanya malipo kwenye biashara na huduma mbalimbali. Kwa miaka ya karibuni huduma za kifedha kwa njia ya simu imekuwa mkombozi kwa wananchi wengi hasa vijijini ikiwapa uwezo wa kuweka akiba, kukopa, bima, huduma ambazo zinachochea ustawi wa jamii. Katika muktadha wa kupanua huduma za mawasiliano na kuyafanya kuwa nafuu zaidi, Serikali imepunguza gharama za kupitisha miundombinu ya mawasiliano kwenye hifadhi ya barabara kutoka USD 1,000 kwa kilomita hadi USD 100 kwa kilomita, hatua itakayorahisisha ufikisha mawasiliano vijijini. Read More

  • AfDB yaunga mkono mkakati wa Rais Samia kwenye kilimo

    Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) inakusudia kuipatia Tanzania TZS bilioni 244 kwa ajili ya kutekeleza programu ya kilimo ya ‘Building A Better Tomorrow-Youth Initiative for Agribusiness (BBT-YIA) na kilimo cha mashamba makubwa kwa mwaka 2023/24. Kupitia programu hiyo iliyoasisiwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Serikali inakusudia kukuza ushiriki wa vijana na wanawake kwenye kilimo kwa kuwawezesha kufanya kilimo endelevu cha kibiashara, pamoja na kuondoa dhana kuwa kilimo hakilipi au kilimo sio kwa ajili ya vijana. Mkakati huo unaendana na malengo ya Serikali ya kukuza sekta ya kilimo kwa kuhakikisha wakulima wananufaika kwa kufanya kilimo cha kisasa, kuwezesha kuongeza akiba ya ya chakula nchini, pamoja na kufungua fursa za ajira kupitia sekta za uzalishaji ikiwemo kilimo, mifugo na uvuvi. Benki hiyo anaendelea kuimarisha mnyororo wa thamani wa kilimo ambapo mbali na fedha hizo imewezesha pia ujenzi wa vituo vya mazao mbalimbali mkoani Dar es Salaam kwa ajili ya kusafirisha nje ya nchi, na vitu vingine mkoani Mbeya, Njombe na Iringa kwa ajili ya matunda na mbogamboga ambavyo vitaanza kutumika mwaka ujao wa fedha. Aidha, kutokana na azma ya Rais ya kukuza kilimo, AfDB inakusudia kuendeleza ushirikiano na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) ambayo inawezesha ujenzi wa miradi ya umwagiliaji pamoja na uongezaji thamani. Read More