-
Faida ya benki za kibiashara nchini imeongezeka kwa TZS bilioni 400 mwaka 2022 na kuvuka ukomo wa shilingi trilioni moja kwa mara ya kwanza katika historia ya sekta ya fedha nchini Tanzania. Kwa mujibu wa taarifa za benki ambazo zimetoa taarifa zao za fedha hadi Januari 30 mwaka huu, zinaonesha kuwa zaidi ta TZS trilioni 1.164 zilikusanywa kama faida (net profit) ikiwa ni ongezeko kutoka TZS bilioni 740 zilizokusanywa mwaka 2021. Ongezeko hilo la faida ambalo limeambatana na kupungua kwa mikopo chechefu, kuongezeka kwa kiwango cha fedha kinachowekwa na wateja wa benki pamoja na mikopo kwa wateja kumetokana kuimarika kwa mazingira mazuri ya biashara nchini chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Benki hizo zimesema kuwa ongezeko hilo la faida ni ishara kuwa ajenda ya Serikali ya kukuza biashara inafanya vizuri ambayo inatokana na usimamizi mzuri ikiwemo wa kisera ambazo zinatoa nafasi kwa sekta binafsi kukua. Ukuaji huo unatarajiwa kuwa na matokeo chanya kwa wananchi kwani unaongeza uwezo wa benki kupanua huduma za kifedha kuwafikia wananchi wengi zaidi lakini pia kuongeza kiwango cha mikopo kwenda sekta binafsi ambayo ina mchango mkubwa kwa maendeleo na kuzalisha ajira. Read More
-
Akiendelea kufanya vizuri kwenye mageuzi ya kiuchumi na kisiasa, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amegeukia sekta ya haki ambapo leo amezindua Tume ya Kuangalia Jinsi ya Kuimarisha Taasisi za Haki Jinai ili kuhakikisha zinatoa haki kwa wananchi wa wakati na kwa misingi ya kisheria. Taasisi ambazo zinakwenda kufanyiwa maboresho ni Jeshi la Polisi, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Jeshi la Magereza pamoja na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya. Wakati wa mapitio tume hiyo itaangalia masuala mbalimbali kwenye taasisi husika ikiwa ni pamoja na mifumo ya utendaji, mafunzo, mifumo ya ajira, matumizi ya TEHAMA, fikra za kiutendaji na mahusiano kati ya taasisi hizo na raia. Katika maboresho hayo Rais Samia anelenga kukomesha vitendo mbalimbali ambavyo vimekuwa vikilalamikiwa na wananchi ikiwa ni pamoja na mamlaka husika kuwabambikia kesi, kucheleweshwa kwa upelelezi, msongamano mkubwa wa mahabusu magerezani, kupambana na rushwa pamoja na kuimarisha uwezo wa taasisi hizo katika kulinda na kutetea maslahi ya nchi kwa kuhakikisha ajira zinatolewa kwa mujibu wa sheria na kunakuwepo mafunzo ya mara kwa mara. Akizungumza wakati wa uzinduzi huo amesema “hakuna kitu kibaya duniani kukichepusha kama haki ya mtu,” na hivyo kama ambavyo hakuna atakaye haki yake ipokonywe, vivyo hivyo anatakiwa kuhakikisha hashiriki katika upokonyaji wa haki ya mwingine. Read More
-
Kupitia mpango wa Building a Better Tomorrow (Ujenzi wa Kesho Bora) Serikali imeanzisha mfuko wa dhamana kwa vijana na huduma za mikopo nafuu chini ya Mfuko wa Pembejeo ili kuwavutia kushiriki katika ukuzaji wa uchumi kupitia kilimo. Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amesema Tanzania imeamua kuanzisha mpango huo kutokana na idadi kubwa ya vijana na wanawake kukosa sifa zinazohitajika na taasisi za fedha wanapoomba mikopo. Zaidi ya theluthi moja (34%) ya Watanzania wakiwa ni vijana ambao ndio nguvu kazi kubwa, Rais Samia amechukua jukumu la kutatua changamoto zao kwenye kilimo, ili kuongeza tija na kuvutia vijana wengi zaidi, ambapo changamoto zilizotatuliwa ni pamoja na mafunzo, upatikanaji wa ardhi, teknolojia na fedha. Kutokana na mkakati wa Rais Samia wa kufanikisha mapinduzi ya kilimo Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) imetangaza kuipatia Tanzania mkopo wa TZS bilioni 280 kwa ajili ya sekta ya kilimo ikiwemo umwagiliaji na kujenga kituo cha usafirishaji na usambazaji mbolea. Tangu kuanzishwa kwa mpango wa BBT miezi sita iliyopita, tayari imetenga zaidi eka 600,000 nchi nzima na shughuli ya kusafisha mashamba hayo inaendelea. Read More
-
Serikali kupitia mpango wa Building a Better Tomorrow inakusudia kuzalisha ajira milioni 1 kupitia kilimo hadi ifikapo mwaka 2025, ambapo mwamko wa vijana kujiunga na programu hiyo itakayowawezesha kupatiwa elimu, mashamba, pembejeo na masoko umekuwa mkubwa. Akishiriki mkutano wa chakula na kilimo wa wakuu wa nchi za Afrika nchini Senegal, Rais amesema mpango huo wa kuvutia vijana kwenye kilimo ambacho kitakuwa cha kibiashara Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amesema hadi Januari 25, 2023 tayari vijana 7,000 wamesajiliwa kujiunga na programu hiyo, kiwango ambacho kimevuka lengo. “Pia tumekuwa tukifanya kazi na benki kwa ajili ya mikopo kwa vijana na wanawake. Tuliweza kupunguza riba kutoka asilimia 15 hadi asilimia tisa,” amesema Rais akibainisha lengo ni kuifanya Tanzania kuwa mfuko wa chakula cha Afrika kupitia nguvu kazi ya vijana ambao ni asilimia 34.5 ya Watanzania wote. #KilimoBiashara Tanzania ya kesho, ni Tanzania ya kilimo cha kisasa kinachofanywa na vijana, na hivi ndivyo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu anavyowezesha vijana. #MamaYukoKazini pic.twitter.com/psP2HkxlxO — Mama yuko Kazini (@mamayukokazini) January 18, 2023 Kupitia mpango huo vijana watapatiwa elimu ya kufanya kilimo cha kibiashara, mashamba yao yatajengewa miundombinu ya umwagiliaji na ghala la kuhifadhi mazao, watapatiwa teknolojia ya kisasa ya uzalishaji, mitaji, pembejeo za kilimo na kuunganishwa na masoko ya mazao yao. Tayari TZS bilioni 3 ambazo zimetengwa kwa ajili ya kufanikisha mpango huo zimeanza kutumika kuwawezesha walengwa lengo likiwa ni kuongeza uzalishaji wa chakula, malighafi, kuzalisha ajira na kubadili fikra na dhana kuwa kilimo hakilipi. Kwa maelezo zaidi namna ya kushirikia katika programu hiyo bonyeza hapa Read More
-
Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan anaendelea kuongeza ajira katika taasisi za Serikali ili kuboresha utoaji huduma kwa wananchi. Read More
-
Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amesema sekta ya kilimo nchini inatarajiwa kukua kwa asilimia 10 ifikapo mwaka 2030 ikilinganisha na ukuaji wa sasa wa takribani asilimia 3.6. Akizungumza kwenye mdahalo wa ‘Food Action Partnership: Investing in Greater Resilience’ nchini Uswisi amesema Tanzania imetengeneza fursa za kitaifa kwa ajili ya mabadiliko ya mfumo wa chakula unaotarajia kuongeza uzalishaji wa chakula, kuimarisha maisha ya watu na kusaidia kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa. Katika kudhibiti mfumo endelevu wa chakula nchini, Rais Samia amesema jitihada kadhaa zimefanyika, ikiwemo kuanzisha mradi kwa ajili ya vijana huku wakiendelea kuimarisha ukuaji wa shoroba za kilimo pamoja na kuongeza bajeti ya kilimo mara 4 ukilinganisha na ile iliyopita. Serikali ya Tanzania inaendelea kutekeleza miradi na mafunzo mbalimbali ya kilimo kwa vijana ili kuongeza tija kwenye kilimo na kuwezesha vijana kushiriki kwenye uchumi wa Tanzania ambapo lengo ni kuzalisha ajira milioni 1 ifikapo mwaka 2025. Mdahalo huo uliohudhuriwa na zaidi ya viongozi 50 kutoka Afrika, Asia, Ulaya na Marekani mbali na Rais Samia wachangiaji wengine walikuwa Rais Gustavo Petro wa Colombia, Tran Hong Ha, Naibu Waziri Mkuu wa Vietnam na Alvaro Lario, Rais wa Wakfu wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Roma. Read More
-
Wafanyabiashara wa kahawa kutoka Tanzania wanaolengeka kuuza kahawa katika soko la China wametakiwa kujisajili kupitia Wizara ya Kilimo nchini Tanzania, ili kukidhi vigezo vya kulifikia soko hilo. Balozi wa Tanzania nchini China, Mbelwa Kairuki amenukuliwa akisema kuwa mabadiliko hayo yatarahisisha usajili wa kampuni za Tanzania zenye nia ya kuuza kahawa katika soko la China ambapo awali kampuni nyingi zilikuwa zikipata changamoto kufanya usajili katika mtandao wa Mamlaka ya Forodha ya China (GACC). Hatua hii ni mwendelezo wa fursa mbalimbali za kiuchumi ambazo Tanzania inaendelea kuzipata tangu Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan alipofanya ziara nchini China ambapo akiwa na mwenyeji wake, Rais Xi Jinping walishuhudia utiaji saini mikataba 15 ya kimkakati inayolenga kuimarisha ushirikiano, biashara na uwekezaji baina ya nchi hizo mbili. Hadi sasa kampuni saba zimeshasajiliwa kuingiza kahawa nchini China ikiwa ni pamoja Kilimanjaro Cables (T) Limited, Cotacof Limited, Taylor Winch Tanzania Limited, Dorman (Tanzania) Ltd, Kamal Agro Limited, Redloong Investment Company Limited na Ibero Coffee Trading Company (T) Limited. Uhakika wa soko la kahawa unaweka uhakika ajira na kuzalisha ajira zaidi kupitia mnyororo wa uongezaji thamani kahawa, soko la uhakika kwa wakulima na kuongeza mapato ya Serikali kwa kuuza bidhaa hiyo nje ya nchi. Wakati Tanzania ikilenga kuongeza uzalishaji wa kahawa kutoka tani 65,235 mwaka 2021/2022 hadi tani 72,000 mwaka 2022/2023, wakati huo huo inalenga kuongeza mauzo yake ya kahawa nchini China na mipango inaendelea kwa wafanyabiashara wa Tanzania kushiriki katika Maonesho ya Uchumi na Biashara ya China na Afrika yanayotarajiwa kufanyika Juni 2023 huko Hunan. Read More
-
Kutokana na mageuzi makubwa yanayoendelea kufanyika nchini kwa kuboresha mazingira ya biashara kupitia mabadiliko ya kisheria na kanuni, ujenzi wa miundombinu na uainishaji maeneo muhimu kwa uwekezaji na biashara, uchumi wa Tanzania kwa mwaka 2023 unatarajiwa kukua kwa asilimia 5 kutoka asilimia 4.7 mwaka 2022. Akizungumza na mabalozi wanaowakilisha nchi zao hapa nchini pamoja na wawakilishi wa mashirika ya kimataifa katika sherehe za mwaka mpya kwa mabalozi (Diplomatic Sherry Party), Mheshimiwa Rais Samia Suluhu amesema mwaka 2022 ulikuwa mwaka wa mageuzi ya kisiasa na kiuchumi ambapo kwa kipindi kifupi cha Julai hadi Novemba kilishuhudia ongezeko la asilimia 22 la miradi iliyosajiliwa nchini kwa kipindi hicho kufikia miradi 132 yenye thamani ya TZS trilioni 7 ambayo itatoa ajira 21,297. “Mabadiliko mbalimbali kupitia Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (Blueprint) yamechochea ukuaji wa sekta binafsi na kurejesha nguvu ya soko na kupunguza mwingilio wa serikali katika shughuli za kiuchumi, jambo ambalo limepelekea kuongezeka kwa uwekezaji nchini,” amesema Rais Samia. Mkakati wa Rais Samia wa kuimarisha sekta binafsi ambayo ina mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa kunawezesha kupunguza tatizo la ajira nchini, kwa vijana wengi kujiajiri na kuajiri kupitia sekta hiyo, kwani takribani vijana milioni 1 huingia kwenye soko la ajira nchini kila mwaka, idadi ambayo Serikali pekee haiwezi kuwahudumia. Kupitia ujenzi wa miradi ya kimkakati unaoendelea nchini ikiwemo Bwawa la Umeme la Julius Nyerere (JNHPP), reli ya kisasa, ujenzi na ukarabati wa meli mbalimbali, bomba la mafuta (EACOP) na mradi wa kuchakata gesi asilia mkoani Lindi, anaamini kuwa uchumi wa Tanzania utaendelea kuimarika na kuwanufaisha Watanzania zaidi. Wakati huo huo, amesema ana imani kuwa kila Mtanzania anayo nafasi katika maendeleo na mustakabali wa Tanzania na kuwa wananchi wanahaki na uhuru ambao wanastahili kuufurahia kwa mujibu wa kanuni na sheria zilizopo nchini. Read More