Mkakati wa Mheshimiwa Rais kuondoka kodi za mabavu waongeza ukusanyaji mapato kwa 38%

Siku chache baada ya kuingia madarakani, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan aliweka wazi msimamo wake kuhusu ukusanyaji wa kodi akiitaka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania kutotumia mabavu na ubabe kukusanya kodi, kwani kufanya hivyo ni kuua biashara na mfumo huo sio endelevu.

“Kodi tunazitaka, na mimi nasema mwende mkakusanye kodi, lakini kodi za dhuluma, hapana, kwa sababu hata hizo hazitatufikisha mbali,” alisistiza Rais na kueleza kuwa anajua kwa uamuzi huo ukusanyaji mapato ungeshuka kwa muda, lakini baada ya muda biashara zikiimarika, makusanyo yatakua.

Miaka miwili tangu kutolewa kwa agizo hilo, Tanzania imeendelea kuweka rekodi ya makusanyo ya kodi, ambapo wastani wa ukusanyaji mapato umeongezeka kutoka TZS trilioni 1.45 kwa mwezi mwaka 2021 hadi TZS trilioni 2 kwa mwezi mwaka 2022, sawa na ongezeko la asilimia 38.

Ukuaji huo umechangiwa na masuala mbalimbali, kubwa likiwa ni kuimarika kwa mazingira ya biashara na uwekezaji ambapo biashara na miradi mipya ya uwekezaji imefunguliwa nchini pamoja na iliyokuwepo kuimarika. Sababu nyingine kuimarika kwa mifumo ya ukusanyaji kodi, kuongezeka kwa uwezo wa walipakodi na kuimarika kwa uhusiano wa TRA na walipakodi.

Kodi ndio nyenzo muhimu inayoiwezesha Serikali kutekeleza majukumu yake ikiwemo kufikisha huduma za kijamii na kimaendeleo kwa wananchi kupitia sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, kilimo, maji na miundombinu.