Uchumi Tanzania

  • Diplomasia ya Uchumi: Mheshimiwa Rais Samia avutia wafanyabiashara zaidi wa Norway kuwekeza Tanzania

    Mwanadiplomasia namba moja wa Tanzania, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu ameendelea kutekeleza kwa vitendo Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania, Diplomasia ya Uchumi, katika ziara zake nje ya nchi kwa kutangaza fursa za biashara na uwekezaji zilizopo nchini pamoja na kukutanisha wafanyabiashara wa ndani na wale wa kimataifa. Matokeo ya mkakati huo yameendelea kuonekana ambapo kwa mwaka 2023 miradi ya uwekezaji iliongezeka kufikia 526 kutoka miradi 293 mwaka 2022, uwekezaji ambapo utazalisha ajira kwa maelfu ya Watanzania, utachochea ukuaji wa biashara, mzunguko wa fedha na kukuza kipato cha mwananchi mmoja mmoja na taifa kwa ujumla. Katika ziara yake ya kihistoria ya kitaifa nchini Norway Mheshimiwa Rais ameendeleza mkakati huo ambapo akizungumza katika Jukwaa la Biashara kati ya Tanzania na Norway ametaja sababu za Tanzania kuwa eneo zuri kwa uwekezaji ikiwa ni pamoja na ukweli kuwa itakuwa moja ya nchi 20 duniani ambazo uchumi wake utakua kwa kasi zaidi mwaka 2024 kwa mujibu wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF). Aidha, sababu nyingine ni amani chini ya demokrasia imara wa mfumo wa vyama vingi wenye kuzingatia tunu za utawala bora, kuheshimu haki za binadamu na utawala wa sheria. Kijiografia, amesema Tanzania inafaa kwa uwekezaji kwani ina Bandari ya Dar es Salaam katika Bahari ya Hindi, inayohudumia mataifa nane na ina usimamizi madhubuti wa uchumi na sera ya fedha. Rais Samia amesisitiza fursa tano za kipaumbele zikiwemo uwekezaji katika nishati mbadala, kilimo, mafuta na gesi, mifuko ya uwekezaji, miundombinu na usafirishaji. Tanzania na Norway zinaadhimisha miaka 60 ya ushirikiano ambapo katika mazungumzo ya Rais Samia na viongozi waandamizi wa taifa hilo wamefikia makubaliano ya kukuza ushirikiano wa kiuchumi kuendana na ukubwa wa historia ya uhusiano uliopo.   Read More

  • Mageuzi ya Mama Yanaendelea: Benki Kuu yaanza utekelezaji sera mpya ya fedha

    Mheshimiwa Rais Samia Suluhu anaendeleza mageuzi chini ya falsafa ya 4R ambapo katika muktadha huo leo Benki Kuu Tanzania (BoT) imetangaza riba elekezi ya asilimia 5.5 ya benki kuu (CBR) kwa benki zote zinazokopa katika benki hiyo ambayo itakatumika kwa robo ya kwanza ya mwaka 2024 kuanzia leo. Mabadiliko hayo yamefuatia taarifa ya BoT ya Januari 3 mwaka huu ambapo ilitangaza kuanza kutumia mfumo unaotumia riba katika kutekeleza Sera ya Fedha, badala ya mfumo unaotumia ujazi wa fedha, mabadiliko ambayo yanalenga kuongeza ufanisi wa sera ya fedha katika kudhibiti mfumuko wa bei na kuimarisha shughuli za kiuchumi. Utofauti wa mfumo wa zamani na wa sasa wa utekelezaji sera ya fedha (hyperlink) Gavana wa BoT, Emmanuel Tutuba amesema kiwango hicho cha riba kimezingatia lengo la kuhakikisha thamani ya shilingi dhidi ya fedha za kigeni inaendelea kuwa imara na kinaendana na malengo ya kuhakikisha kuwa mfumuko wa bei unabaki ndani ya lengo la asilimia 5 na kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi kufikia lengo la asilimia 5.5 au zaidi kwa mwaka 2024. Kupitia mfumo mpya, pamoja na mambo mengine BoT inatekeleza majukumu yake kwa kupandisha au kushusha kiwango cha riba kwa mikopo kwenda benki za kibiashara, ili kuongeza au kupunguza fedha kwenye mzunguko, kudhibiti mfumuko wa bei, kuimarisha thamani ya shilingi au kukabiliana na changamoto nyingine ya kiuchumi kwa wakati husika. Mfumo unaotumia riba unatumika katika nchi zote za Afrika Mashariki kama sehemu ya mkakati wa kuwa na sarafu moja na benki kuu moja ya Afrika Mashariki, pia unatumika katika jumuiya nyingine za kiuchumi ambazo Tanzania ni mwanachama.     Read More

  • Mikakati ya Rais Samia unavyoweka rekodi ya uwekezaji Tanzania

    Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kimesajili miradi ya uwekezaji 229 yenye thamani ya TZS trilioni 4.5 kati ya Januari hadi Juni mwaka huu, ambapo lengo ni kufikia miradi 400 ifikapo Desemba 2023. Idadi hiyo inadhihirisha kasi kubwa ya usajili wa miradi nchini ikilinganishwa na miradi 293 iliyosajiliwa mwaka 2022, hivyo kusajili asilimia 78 ya miradi hiyo ndani ya nusu mwaka ni mafanikio makubwa kwa nchi. Kusajiliwa kwa miradi hiyo inayotoa ajira zaidi ya 30,000 kwa Watanzania katika sekta mbalimbali ni matokeo ya sera ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini, ikiwemo kuboresha sheria, kupunguza tozo/kodi mbalimbali na kuimarisha amani na utulivu. Aidha, takwimu zinaonesha mkakati huo wa Rais umefanikiwa zaidi kwani kwa miaka sita ya Serikali ya awamu ya tano, jumla ya miradi ya TZS trilioni 45 ilisajiliwa, huku miaka miwili ya Serikali ya awamu ya sita ikisajili miradi ya trilioni 22 ndani ya miaka miwili, takwimu zinazoonesha kuwa itafanya vizuri kuliko awamu iliyopita. Aidha, sababu nyingine ni taasisi 12 za usimamizi kuwa katika jengo moja hivyo kurahisisha utoaji huduma pamoja na matumizi ya TEHAMA yaliyorahisisha utoaji wa leseni na vibali mbalimbali vya biashara na uwekezaji hasa kupitia dirisha ya kielektroniki ambapo mwekezaji sasa anaweza kuwasilisha maombi akiwa popote dunia Read More

  • Rais Samia airejesha Tume ya Mipango kwa sura mpya ili kuchochea maendeleo nchini

    Serikali chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan anaiunda upya Tume ya Mipango ambayo itakuwa chini ya Rais ikiwa na jukumu la kubuni, kupanga, kuratibu na kusimamia mipango ya maendeleo ili kuwa na mfumo jumuishi wa ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa vipaumbele vya maendeleo ya Taifa. Kuunda upya kwa tume hiyo na kuiweka chini ya Rais ni kuendelea kuyaishi maono ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ambaye kwa mara ya kwanza alianzisha mwaka 1962 ikiwa ni idara ambapo wakati wa uanzishaji wake walisema “Nakusudia kuanzisha idara mpya, idara ya mipango ya maendeleo, idara hiyo itakuwa chini yangu mwenyewe.” Uamuzi wa Rais kurejesha tume hiyo utawezesha uwepo wa utaratibu wa kupanga pamoja mipango ya kisekta, hususani sekta zenye majukumu yanayotegemeana na kuwa na mfumo wa kisheria na chombo mahsusi cha kusimamia uandaaji, utekkelezaji wa mipango ya maendeleo, utafiti na kuishauri Serikali kuhusu vipaumbele vya maendeleo ya Taifa. Majukumu haya kwa sasa yanatekelezwa na Wizara ya Fedha na Mipango, lakini kumekuwepo na changamoto ya miradi inayoendana kutekelezwa kwa nyakati tofauti sehemu husika, mfano barabara inajengwa baada ya muda inavunjwa ili kupitisha bomba la maji. Hivyo kuwepo kwa tume maalum chini ya ofisi ya Rais kutaondoka mkanganyiko huo ili miradi kama hiyo itekelezwe kwa wakati mmoja ili kuleta ufanisi na kuipunguzia serikali gharama zisizo za lazima. Aidha, tofauti na tume iliyokuwepo awali ambayo ilikuwa ikiendeshwa kwa hati idhini (instruments) tume mpya itakuwa na hadhi ya kisheria ambayo itaipa tume nguvu zaidi na kulinda mawazo yanayotolewa na kuleta utofauti katika mfumo wa uendeshaji. Read More

  • Matunda ya mikakati ya kiuchumi ya Rais Samia yanavyozidi kuonekana

    Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) limetoa takwimu zinazoonesha kuongezeka kwa pato la Taifa la Tanzania kutoka Dola za Marekani Bilioni 69.9 (TZS trilioni 163.5 trilioni) kwa mwaka 2021, wakati ambapo Rais Samia alipoingia madarakani hadi kufikia Dola za Marekani Bilioni 85.42 (TZS trilioni 200) kwa mwaka huu wa 2023, Huu ni ukuaji mkubwa zaidi katika kipindi cha muda mfupi cha uongozi wa awamu ya sita chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ambapo ndani ya miaka miwili pato hilo limeongezeka kwa Dola za Marekani Bilioni 16 (TZS trilioni 37.616) ikilinganishwa na ukuaji wa miaka sita ya awamu ya tano ambapo pato hilo lilikua kwa Dola za Marekani Bilioni 12 pekee (TZS trilioni 28.212). Vilevile IMF imeonesha kuwa kwa mwenendo uliopo hadi mwaka 2028 Tanzania kutakuwa na watu milioni 73.36 huku pato la Taifa likitarajiwa kukua hadi dola bilioni 136.09 (TZS trilioni 318.8) na pato la mtu mmoja mmoja likitarajiwa kukua hadi dola 1,860 (TZS milioni 4.3), huku kasi ya ukuaji wa uchumi ikitarajiwa kuwa asilimia 7. Ukuaji huu wa uchumi ni matokeo ya jitihada za makusudi za Mheshimiwa Rais ambapo tangu alipoingia madarakani Machi mwaka 2021, ametekeleza sera rafiki kwa sekta binafsi, ambayo imeongeza kasi ya uwekezaji, biashara na ukuaji wa uchumi nchini huku akifungua fursa za ajira kwa wananchi kote nchini. Kazi hii kubwa ya ukuaji wa uchumi ni utekelezaji wa ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambayo inaeleza lengo la kukuza kwa Pato la Taifa pamoja na kujenga uchumi wa kisasa, shirikishi na shindani, utakaowezesha ustawi wa wananchi. Read More