Mfumuko wa Bei

  • IMF yaipongeza Tanzania kwa hatua za kisera zilizodhibiti mfumuko wa bei

    Shirika la Kimataifa la Fedha (IMF) limeipongeza serikali ya Tanzania kwa kuimarisha utulivu wa kiuchumi wakati ambapo dunia ilikuwa inapitia changamoto mbalimbali ikiwemo janga la Ugonjwa wa Virusi vya Korona (UVIKO-19), vita vya Urusi na Ukraine na mabadiliko ya tabianchi. Pongezi hizo zimetolewa na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa IMF, Bo Li baada ya kumaliza ziara yake nchini ambapo amesema “jitihada za haraka za serikali ya Tanzania zilisaidia kudhibiti mfumuko wa bei na kulinda uchumi dhidi ya athari za vita nchini Ukraine.” Licha ya mafanikio hiyo, taasisi hiyo imeihimiza Tanzania kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya ndani ambayo yatakuza uwezo wa Serikali katika kugharamia huduma za kijamii na kuongeza uwekezaji katika elimu, afya, maji na sekta nyingine muhimu. Li akizungumza na wawakilishi wa sekta binafsi, asasi za kiraia na wadau wengine wa maendeleo ameeleza kuvutiwa sana na nguvu na uhai wa uchumi wa Tanzania. Tanzania ni moja ya nchi chache barani Afrika zenye kiwango cha chini zaidi cha mfumuko wa bei ambapo kwa miezi sita mfululizo umekuwa ukishuka kutoka asilimia 4.9 Januari hadi asilimia 3.6 Juni mwaka huu. Read More

  • Benki ya Dunia: Tanzania ni nchi ya mfano katika usimamizi wa uchumi

    Benki ya Dunia imeimwagia sifa Tanzania chini Rais Rais Samia Suluhu Hassan kwa usimamizi mzuri wa uchumi na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayopata fedha kutoka kwenye taasisi hiyo ikilinganishwa na nchi nyingine nyingi za Afrika. Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Dunia anayesimamia Kundi la Kwanza la nchi za Kanda ya Afrika (Africa Group 1 Constituency), Dkt. Floribert Ngaruk amesema Tanzania ni nchi ya mfano katika usimamizi wa sera za uchumi na fedha ambapo licha ya changamoto za UVIKO-19 na vita inayoendelea baina ya Urusi na Ukraine, tathimini ya benki hiyo inaonesha kuwa uchumi wa Tanzania uko imara ikilinganishwa na nchi nyingine za Afrika. “Tanzania ni nchi ya kupigiwa mfano kwa usimamizi mahiri wa masuala ya uchumi mpana, si tu kwa nchi za Afrika Mashariki, bali kwa nchi za Afrika, ambapo kiwango cha ukuaji uchumi cha wastani wa asilimia 5.4 ni cha juu, na ninawapongeza sana” amesema Dkt. Ngaruko Aidha, amepongeza uhusiano imara uliopo kati ya Tanzania na Benki ya Dunia na kuahidi kuwa benki yake itaendelea kuisaidia Tanzania katika jitihada zake za kukuza uchumi na kuwaondolea umasikini wananchi wake kwa kusaidia fedha zitakazotumika kutekeleza miradi mbalimbali ya kiuchumi na kijamii pamoja na kutoa misaada ya kiufundi. Mpaka sasa Benki ya Dunia imewekeza zaidi ya TZS trilioni 16.7 kwa ajili ya kutekeleza miradi zaidi ya 29 nchini ambapo kati ya miradi hiyo, 24 yenye thamani ya TZS trilioni 15 ni ya kitaifa, na mingine 5 yenye thamani ya TZS trilioni 1.7 ni ya kikanda. Read More