Benki ya Dunia

  • Tanzania ya pili Afrika matumizi ya TEHAMA kuhudumia wananchi

    Tanzania imetajwa na Benki ya Dunia (WB) kuwa nchi ya 26 duniani na ya pili barani Afrika kwa kuwa na mfumo madhubuti wa matumizi ya Teknolojia ya Mawasiliano na Habari (TEHAMA) katika kutoa huduma kwa wananchi, utaratibu ambao unawezesha huduma kupatikana kwa wakati na unafuu. Katika utafiti huo wa GovTech Maturity Index (GTMI) 2022 uliofanywa na Benki ya Dunia na kuhusisha nchi 198 umeiweka Tanzania katika Kundi A ikipanda kutoka Kundi B mwaka 2021 ambapo kwa dunia ilikuwa nafasi ya 90 na Afrika nafasi ya tano, ambapo matumizi ya TEHAMA yamekuwa kwa asilimia 0.86 kwa mwaka uliopita. Tanzania imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuimarisha matumizi ya teknolojia ya kidijitali kwenye kutoa huduma kwa umma, ambapo hivi karibuni Rais Samia Suluhu Hassan alishuhudia utiaji saini mikataba ambayo itakwenda kufikisha huduma ya mawasiliano kwa Watanzania zaidi ya milioni 8, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati huo. Utafiti huo umeonesha kuwa sekta za elimu, afya, huduma za fedha kwa simu na kilimo ndizo sekta zinazoongoza kutoa huduma kwa umma kwa kutumia TEHAMA. Mkakati huo umeendelea kufanikiwa kutokana na hatua za Serikali kuweka mazingira rafiki na kuwainua wabunifu wa kidijitali. Kufikishwa kwa mawasiliano kwenye vijiji ambavyo havikuwa na huduma hiyo hapo awali kutapanua zaidi wigo wa Watanzania wanaoweza kunufaika na huduma za kidijitali za Serikali, na hivyo kukuza kiwango cha Tanzania kwa upande wa Afrika na dunia katika tafiti zijazo. Read More

  • Benki ya Dunia: Tanzania ni nchi ya mfano katika usimamizi wa uchumi

    Benki ya Dunia imeimwagia sifa Tanzania chini Rais Rais Samia Suluhu Hassan kwa usimamizi mzuri wa uchumi na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayopata fedha kutoka kwenye taasisi hiyo ikilinganishwa na nchi nyingine nyingi za Afrika. Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Dunia anayesimamia Kundi la Kwanza la nchi za Kanda ya Afrika (Africa Group 1 Constituency), Dkt. Floribert Ngaruk amesema Tanzania ni nchi ya mfano katika usimamizi wa sera za uchumi na fedha ambapo licha ya changamoto za UVIKO-19 na vita inayoendelea baina ya Urusi na Ukraine, tathimini ya benki hiyo inaonesha kuwa uchumi wa Tanzania uko imara ikilinganishwa na nchi nyingine za Afrika. “Tanzania ni nchi ya kupigiwa mfano kwa usimamizi mahiri wa masuala ya uchumi mpana, si tu kwa nchi za Afrika Mashariki, bali kwa nchi za Afrika, ambapo kiwango cha ukuaji uchumi cha wastani wa asilimia 5.4 ni cha juu, na ninawapongeza sana” amesema Dkt. Ngaruko Aidha, amepongeza uhusiano imara uliopo kati ya Tanzania na Benki ya Dunia na kuahidi kuwa benki yake itaendelea kuisaidia Tanzania katika jitihada zake za kukuza uchumi na kuwaondolea umasikini wananchi wake kwa kusaidia fedha zitakazotumika kutekeleza miradi mbalimbali ya kiuchumi na kijamii pamoja na kutoa misaada ya kiufundi. Mpaka sasa Benki ya Dunia imewekeza zaidi ya TZS trilioni 16.7 kwa ajili ya kutekeleza miradi zaidi ya 29 nchini ambapo kati ya miradi hiyo, 24 yenye thamani ya TZS trilioni 15 ni ya kitaifa, na mingine 5 yenye thamani ya TZS trilioni 1.7 ni ya kikanda. Read More