Miaka Miwili ya Mama

  • #MiakaMiwiliYaMama: Ajira za moja kwa moja Watanzania zaidi ya 85,000

    Mkakati wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan wa kuboresha mazingira ya biashara nchini na kuvutia uwakezaji umezaa matunda ambapo takwimu kutoka Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) zinaonesha kuwa thamani ya uwekezaji nchini umekua kwa asilimia 173. Ripoti ya TIC inaonesha kuwa thamani ya uwekezaji imepanda kufikia TZS trilioni 19.87 katika miaka miwili ya Serikali ya awamu ya sita, kutoka TZS trilioni 7.27 iliyorekodiwa katika miaka miwili kabla hajaingia madarakani. Ongezeko hilo ni matokeo ya kazi kubwa ya Rais ya kurejesha imani ya wawekezaji ndani na nje ya nchi ambao amekuwa akikutana katika ziara zake nje ya nchi na ndani ya nchi ambapo pamoja na kutangaza fursa za uwekezaji, pia alizipatia ufumbuzi changamoto zilizowakabili. Kati ya Machi 2021 na Februari 2023 idadi ya miradi iliyosajiliwa imeongezeka kutoka 455 hadi 575, ambayo ni sawa na ongezeko la asilimia 26. Kati ya miradi hiyo, asilimia 32 inamilikiwa na Watanzania, asilimia 42 ni ya wageni na asilimi 27 ni ubia kati ya wageni na wazawa. Kutokana na uwekezaji huo, idadi ya ajira zilizozalishwa kwa Watanzania zimeongezeka kutoka 61,900 hadi 87,187, uwekezaji mkubwa ukiwa kwenye sekta za viwanda, ujenzi wa majengo ya kibiashara na usafirishaji. Mafanikio haya yamehusishwa pia na Tanzania kushiriki katika mikutano ya kimataifa. Read More

  • #MiakaMiwiliYaMama: Amewajengea vijana uwezo wa kujiajiri kupitia kilimo

    Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan anadhihirisha kwa vitendo kauli yake aliyotoa kuwa hataki kuingia katika historia ya kuwa mmoja wa wanaowalaumu vijana kuwa hawajiajiri, badala yake anawawekea mazingira wezeshi ya kujiajiri kupitia kilimo ambapo lengo ni kuzalisha ajira milioni 3, kipaumbele kikiwa vijana na wanawake. Machi 20 mwaka huu amezindua mashamba ya pamoja (Block Farms) zaidi ya ekari 12,000 ambazo zitagawawiwa kwa vijana, kila mmoja kwa ukubwa usiozidi ekari 10, pia alizindua ndege zisizo na rubani, mashine za umwagiliaji na magari kwa ajili ya maafisa wa wilaya ili kuhakikisha vijana popote walipo nchini wanapata usaidizi wa kitaalamu katika kufanya kilimo cha kibiashara. Katika azma ya kukifanya kilimo kuwa cha vijana, ameahidi kuendelea kutenga bajeti mahsusi kwa ajili ya watendaji kwenye sekta ya kilimo ili shughuli zote zifanyike kwa usasa kuanzia uzalishaji hadi uuzaji mazao na bidhaa. “Tunasema ni kilimo cha vijana, hivyo vijana wawepo shambani, wawepo kwenye utaalamu, wawepo kwenye kuendesha mitambao, sehemu zote kuwa na vijana wanaokwenda kwenye sekta ya kilimo,” amesema akizindua programu ya Building a Better Tomorrow. Katika miaka miwili ya uongozi wake, kilimo ni moja tu ya njia anazotumia kumwinua kijana wa Kitanzania na kukabiliana na changamoto ya ajira inayoisumbua dunia. Ujenzi wa vyuo vya ufundi stadi katika kila wilaya, mikopo ya halmashauri, kuboresha mazingira ya biashara hasa kwa wajasiriamali ni maeneo mengine ambayo yametoa ajira kwa vijana wengi. Read More

  • #MiakaMiwiliYaMama: Fursa zaidi kwa vijana, sasa Serikali kuwapatia pembejeo za kilimo

    Katika moja ya hotuba zake kwa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere alieleza umuhimu wa kubadili mfumo wa kilimo nchini akisema kuwa kilimo cha kutegemea mvua, kisicho na mbolea, dawa na maarifa, hakitusaidii sana. Anayoyafanya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Kupitia Mfuko wa Pembejeo za Kilimo (AGITF) ni kuyaishi maono ya Mwalimu Nyerere kwani anakuza kilimo kwa kuwapatia vijana pembejeo (dawa, mbegu bora, viuatilifu), ili kubadili kilimo na kufikia lengo la kumnufaisha mkulima, kukuza mchango wake kwenye uchumi, kuongeza uzalishaji wa chakula na malighafi za viwandani. Kama hilo halitoshi, Machi 20 mwaka huu Rais atazindua programu ya Building a Better Tomorrow – Youth Agribusiness Initiative (BBT-YIA) ambapo katika awamu ya kwanza vijana 812 watapatiwa mafunzo kwa miezi minne bure, kisha watapewa mashamba ambayo tayari yamewekewa mifumo ya umwagiliaji kwa ajili ya kilimo. Ikiwa kati ya Watanzania 10, saba wanajishughulisha na kilimo, na ikiwa vijana ndio nguvu kazi kubwa, uamuzi wa Rais kuwekeza kwa vijana kwenye kilimo utabadili dhana kuwa kilimo hakilipi, kilimo ni cha wazee na changamoto ya ajira ambayo inawakabili vijana duniani kote itapungua nchini. Rais ametoa wito wa sekta binafsi na taasisi za kimataifa kushirikiana na Serikali katika kuwawezesha vijana na wanawake, hasa kuwapatia mitaji ya shughuli za kilimo, uvuvi na ufugaji ili kuwawezesha kufikia malengo binafsi na ya kitaifa. Read More

  • #MiakaMiwiliYaMama na Diplomasia ya Uchumi: Shilingi ya Tanzania kutumika kununua bidhaa nchini India

    Azma ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu kuimarisha diplomasia ya uchumi na kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji inazaa matunda ambapo Tanzania na India zimefikia makubaliano ya kibiashara ambayo yatawezesha wafanyabiashara kutoka pande zote kutumia fedha zao (shilingi na rupia) katika kufanya miamala ya kibiashara. Nafasi hii itarahisisha biashara ambapo India ni moja ya washirika wakubwa wa kibiashara na Tanzania ambapo thamani ya biashara kati ya nchi hizi ni TZS trilioni 10.4 katika mwaka ulioishia Machi 2022. Takwimu zinaonesha kuwa katika mwaka wa kwanza wa Rais Samia, India iliingiza nchini bidhaa zenye thamani ya TZS trilioni 5.3, huku ikipokea bidhaa za TZS trilioni 5.1 kutoka Tanzania. Utaratibu huu mpya si tu utakuza biashara kati ya mataifa haya kufikia lengo la zaidi ya TZS trilioni 13.8 mwaka huu, bali pia utaziwezesha kutunza akiba ya fedha za kigeni ambao sasa hazitahitajika kufanya miamala. Watanzania wanaofanya kazi katika sekta za kilimo na madini watanufaika zaidi kutokana na sekta hizo kuingiza bidhaa zaidi nchini India. Kwa mujibu wa wachumi na wataalamu wa biashara, uamuzi huo pia utaimarisha utabirikaji wa viwango vya ubadilishaji wa fedha za kigeni jambo ambalo ni la muhimu sana katika biashara za kimataifa kwani ina usimamizi wa fedha yake tofauti na awali ilipokuwa ikitumia dola za Marekani. Read More