Sekta ya Utalii

  • Rais Dkt. Samia atunukiwa tuzo ya kimataifa kukuza sekta ya utalii

    Utendaji kazi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan umeendelea kutambulika kimataifa ambapo siku chache tangu atajwe miongoni mwa wanawake 100 wenye nguvu zaidi duniani kwa mwaka wa pili mfululizo, sasa ametunukiwa tuzo ya Mwongozaji Bora wa Watalii, tuzo iliyotolewa na Taasisi ya Kimataifa ya International Iconic Awards ya nchini India. Taasisi hiyo imemtunuku Dkt. Samia tuzo hiyo kutokana na mchango wake katika uandaaji wa filamu ya Tanzania: The Royal Tour ambayo imekuwa na mchango mkubwa sana katika kukuza sekta ya utalii, hasa baada ya kuathiriwa na janga la UVIKO19 tangu mwaka 2019. Akipokea tuzo hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Pindi Chana amesema itaipa Serikali ari ya kuendelea kuboresha sekta ya utalii ambayo imeendelea kukua ambapo mwaka 2021 Tanzania ilipokea watalii 992,692 lakini mwaka 2022 tayari imepokea watalii zaidi ya milioni 1, huku wengine wakiendelea kuingia. Mbali na kutangaza utalii filamu hiyo imeonesha fursa za biashara na uwekezaji zilizomo nchini ambapo wafanyabiashara na wawekezaji kutoka mataifa mbalimbali, ikiwemo Marekani, wamefika nchini kwa ajili ya kuangalia fursa za biashara na uwekezaji. Read More