Mama Yukokazini
-
AKIAHIDI, ANATIMIZA. Hayo ndiyo maneno mawili yanayoweza kutumika kueleza tukio la Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuzindua Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 (Toleo la Mwaka 2024), ambayo ni ahadi aliyoitoa Aprili 2021 wakati akihutubia bunge, mwenzi mmoja baada ya kuingia madarakani. Akizungumza bungeni alisema kuwa serikali itaifanyia maboresho sera hiyo ili iendane na mabadiliko ambayo yametokea ndani na nje ya nchi katika sekta mbalimbali. Ikiwa ni miaka 24 tangu kupitishwa kwa sera hiyo, leo Mei 19, 2025 Mheshimiwa Rais amezindua toleo hilo ambalo limejikita katika Diplomasia ya Uchumi likilenga kulisukuma Taifa mbele na kuimarisha ushiriki na ushindani katika siasa na maendeleo ya kimataifa, kulinda na kutetea maslahi ya Tanzania kupitia diplomasia makini na shirikishi. Toleo la mwaka 2024 limeleta maboresho mbalimbali ambayo ni pamoja na kuongeza msingi mmoja (wa nane) katika Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania. Msingi huo ni kulinda na kuendeleza maadili, mila na utamaduni wa Mtanzania ikiwemo kukuza matumizi ya lugha ya Kiswahili, hatua ambayo inalenga kukabiliana na uvamizi mkubwa wa utamaduni na ustaarabu unaoendelea. Aidha, mambo mengine manne yaliyoongezwa ni, moja, kuimarisha Diplomasia ya Uchumi kwa kuvutia uwekezaji wa mitaji mikubwa, kutumia vizuri fursa ya kijografia tuliyojaliwa na kufaidika na soko huru la biashara Afrika. Pili, ni matumizi ya lugha ya Kiswahili kama nyenzo ya kujenga ushawishi ili kupanua masoko ndani na nje ya Afrika. Tatu, kukuza ushiriki wa Diaspora katika kukuza uchumi wao binafsi na uchumi wa taifa, na nne ni kuangalia fursa mpya za ushirikiano wa kiuchumi ikiwemo uchumi wa buluu ili kuchochea ukuaji wa kiuchumi. Ametumia nafasi hiyo kuwapongeza wote walioshiriki kuandaa sera hiyo, hasa wananchi waliotoa maoni akisema kuwa “mmeshiriki katika kujenga hatma ya nchi yenu na mmeweka alama isiyofutika.” Read More
-
Falsafa ya 4R (Reconciliation, Resilience, Reform, and Rebuild) ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuleta mageuzi katika sekta mbalimbali zinazogusa maisha ya Watanzania na kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchini. Moja ya sekta hizo ni uchukuzi, ambapo Mageuzi (Reform) yaliyofanywa katika Bandari ya Dar es Salaam kwa kuingia ubia na Kampuni za DP World na Tanzania East Africa Gateway Terminal Limited (TEAGTL) katika kuendeleza na kuendesha baadhi ya maeneo ya bandari hiyo yameendelea kuleta matokeo, ikiwemo kuongeza mapato. Kati ya Julai, 2024 hadi Februari 2025, mapato yatokanayo na Kodi ya Forodha kutoka bandarini yanayokusanywa kutokana na shughuli za kibandari yamefikia TZS trilioni 8.26, ambalo ni ongezeko la TZS trillion 1.18 ikilinganishwa na makusanyo ya TZS trilioni 7.08 yaliyokusanywa kipindi kama hicho kwa mwaka 2023/24. Mafanikio hayo yametokana na wawekezaji hao kuwezesha upatikanaji wa vifaa na mitambo ya kisasa na mifumo ya TEHAMA inayoendelea kuleta ufanisi katika uendeshaji wa shughuli za kibandari, hasa kuondoa msongamano wa mizigo na foleni za meli, hali inayochochea wafanyabiashara zaidi kuchagua kutumia bandari hiyo, hivyo kuongeza mapato. Lengo la Mheshimiwa Rais Samia kushirikisha sekta binafsi ni kuongeza tija katika utendaji wa bandari nchini ili kuziwezesha zichangie zaidi katika ukuaji wa uchumi wa Taifa letu na maendeleo ya wananchi kwa ujumla kwa kuwafanya wanufaike na rasilimali za nchi yao. Read More
-
Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kuleta mageuzi makubwa katika sekta mbalimbali nchini ambapo katika sekta ya maji, ndani ya kipindi cha miaka minne amekamilisha miradi ya maji zaidi ya 2,331 mijini na vijijini ambayo imefikisha maji kwa mamilioni ya wananchi. Kutokana na ufanisi huo asilimia 83 ya wakazi wote wa vijijini wanapata maji safi na salama ikiwa ni ongezeko toka asilimia 72.3 alizokuta wakati anaingia madarakani Machi 2021. Aidha, kwa sasa asilimia 91.6 ya wananchi wa mijini wanapata huduma ya maji safi na salama ikilinganishwa na wastani wa asilimia 86 aliyoikuta. Mafanikio haya yanakaribia lengo lililoanishwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (2020-2025) ambayo inaielekeza serikali kuongeza kasi ya usambazaji majisafi na salama ili kutosheleza mahitaji kwa zaidi ya asilimia 85 vijijini na zaidi ya asilimia 95 kwa mijini, kwa upande wa Tanzania Bara, ifikapo Desemba 2025. Ili kuhakikisha lengo la ilani, Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi ya maji 1,544. Hatua hii inadhihirisha dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Rais kufikisha maji kwa kila mwananchi popote alipo akitambua kuwa maji ni uhai, maendeleo na usalama kwa wananchi. Read More
-
Ni furaha furi furi kama sio furaha bojo bojo kwa watumishi wa umma na Watanzania kwa ujumla baada ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kutangaza nyongeza ya kima cha chini cha mshahara kwa asilimia 35.1. Kutokana na nyongeza hiyo, kima cha chini kuanzia Julai 1, 2025 kitakuwa TZS 500,000 toka kiwango cha TZS 370,000 cha sasa. Mheshimiwa Rais ametangaza neema hiyo katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Dunia (Mei Mosi) ambayo kitaifa imefanyika mkoani Singida ikiwa na kaulimbiu isemayo, “Uchaguzi Mkuu 2025 utuletee viongozi wanaojali haki na maslahi ya wafanyakazi wote, sote tushiriki.” Amesema nyongeza hiyo ni sehemu ya hatua ambazo serikali yake imeendelea kuchukua kuleta ustawi kwa wafanyakazi nchini, na kwamba uamuzi huo umewezeshwa na kasi ya ukuaji wa uchumi kupanda hadi kufikia 5.5% kwa mwaka, hali iliyochangiwa na wafanyakazi kujituma na kufanya kazi kwa bidii. Kupitia mitandao ya kijamii wananchi wamefurahia nyongeza hiyo ambapo wameandika jumbe za kumpongeza. Baadhi ya jumbe hizo ni; “Nakuamini na nakupenda sana mama maisha yangu yote sijawahi kupiga kura ila mwaka huu inshallah nna Imani kura yangu unayo ya kwanza kwenye maisha yangu,”- Hamoud Jimia. “Ubarkiwe mama ikulu yako huna mpinzani hata kidgo,”- Kisila Legandy “Safi mama Samia, wewe ndo unatudai na tunakuhakikishia lazima tukulipe,”- Julius Peter “Kima cha chini cha mashahara kinapanda kutoka 300k mpaka 500k nomaa,”- Msaki. Kuhusu sekta binafsi Mheshimiwa Rais amesema kuwa Bodi ya Kima cha Chini cha Mshahara inaendelea na tathmini kwa lengo la kuboresha viwango vya mishahara kwa sekta binafsi. “Tutaendelea kuboresha mazingira ya wafanyakazi ikiwemo maslahi ya wafanyakazi kwa kadiri hali itakavyoruhusu… Ili tuweze kujenga vyema Taifa letu ni lazima tulinde amani na utulivu nchini,” amesisitiza Rais Dkt. Samia. Read More
-
Isome hapa hotuba ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika maadhimisho ya Miaka 61 ya Muungano wa Tanzania. Read More
-
Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA imevunja rekodi ya makusanyo tangu kuanzishwa kwake kwa kukusanya Shilingi Trilioni 3.587 kwa Mwezi wa Desemba sawa na asilimia 103.52 ya lengo ambalo lilikuwa ni kukusanya Shilingi Trilion 3.465. Makusanyo hayo ni sawa na ukuaji wa asilimia 17.59 ukilinganisha na kiasi cha Shilingi Trilioni 3.050 zilizokusanywa mwezi Desemba mwaka 2023. Taarifa iliyotolewa TRA imeeleza kuwa mbali na kuvuka malengo ya Mwezi Desemba katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka wa fedha 2024/2025 (Oktoba-Desemba 2024) imefanikiwa kukusanya kiasi cha Shilingi Trilioni 8.741 sawa na ufanisi wa asilimia 104.63 ya lengo la kukusanya Shilingi Trilioni 8.354 ambayo ni sawa na ukuaji wa asilimia 19.05 ukilinganisha na kiasi cha Shilingi Trilioni 7.342 zilizokusanywa katika kipindi kama hicho mwaka wa fedha 2023/24. Vilevile TRA imeandika rekodi mpya ya kuweza kufikia na kuvuka lengo la makusanyo kwa miezi sita mfululizo katika nusu ya kwanza ya mwaka wa fedha 2024/2025. Kamishna Mkuu wa TRA Bwn. Yusuph Mwenda amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapa miongozo mizuri iliyowawezesha kukusanya kodi kwa hiari na kuvuka malengo. Read More
-
Serikali imetangaza wanafunzi wote 974,332 wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka 2025 bila kusubiri machaguo kama ilivyokuwa ikifanyika miaka iliyopita. Kwa miaka kadhaa iliyopita ilizoeleka wanafunzi waliohitimu darasa la saba aidha kushindwa kujiunga au kujiunga na elimu ya sekondari kwa mafungu kutokana na sababu mbalimbali lakini chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan suala hilo limefikia ukomo. Kwa mujibu wa taarifa kutoka Ofisi ya Rais-TAMISEMI wanafunzi wote waliofaulu wataanza masomo kwa wakati mmoja ikiwa ni matokeo ya maandalizi ya mapema yaliyofanywa na Serikali ili kuhakikisha kuwa wanafunzi wote watakaofaulu mtihani wa kumaliza darasa la saba mwaka 2024 wanajiunga na elimu ya sekondari ifikapo Januari 13, 2025. Miongoni mwa shughuli za maandalizi zilizofanyika ni kujenga na kuboresha miundombinu ya shule ikiwemo vyumba vya madarasa, nyumba za walimu pamoja na uwepo wa madawati na walimu wa kutosha ikikukmbukwa kuwa serikali imetangaza ajira mpya za walimu 3,633 hivi karibuni. Kati ya wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza wasichana ni 525,225 na wavulana ni 449,107. Read More
-
Jumapili, Desemba mosi, 2024 katika Ikulu ndogo ya Arusha, Rais wa Jamhuri ya Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amekutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa kisiasa na wa kimila wa jamii ya Kimaasai (Malaigwanani) wanaoishi eneo la Ngorongoro na maeneo ya jirani. Mkutano huo umefanyika kwa lengo la kuwasikiliza viongozi hao kufuatia kuwepo kwa malalamiko dhidi ya baadhi ya maamuzi ya Serikali yanayohusu eneo la Ngorongoro. Katika mazungumzo hayo Rais Dkt. Samia amesema ataunda Tume mbili ambapo moja itachunguza na kutoa mapendakezo kuhusu masuala ya ardhi yanayolalamikiwa na wakazi wa Ngorongoro na nyingine itaangalia utekelezaji wa zoezi zima la uhamiaji kwa hiari kutoka eneo la Hifadhi ya Ngorongoro. Rais Dkt. Samia amewahakikishia kuwa Serikali itaendelea kuimarisha utendaji kazi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NCAA) kwa lengo la kuimarisha mahusiano kati ya Serikali na jamii hiyo huku pia akisisitiza ulazima wa wananchi kushirikishwa ipasavyo katika upangaji na utekelezaji miradi inayopita kwenye maeneo yao. Aidha, Rais Dkt. Samia amesisitiza kuwa Tanzania ni nchi inayojivunia umoja wa kitaifa na yenye Serikali inayowahudumia Watanzania wote. Hivyo, ameitaka Ofisi ya Rais TAMISEMI kushughulikia changamoto zinazojitokeza ikiwemo kukosekana kwa baadhi ya huduma za msingi za kijamii katika eneo la Ngorongoro. Read More
-
Zaidi ya mashabiki 60,000 walioujaza Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam walilipuka kwa shangwe baada ya mwamuzi kupuliza filimbi ya kumaliza mchezo dhidi ya Guinea na kuibuka na ushindi wa goli 1-0, ushindi uliomaanisha kuwa Tanzania kwa mara ya nne imefuzu kushiriki michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 itakayofanyika nchini Morroco Tanzania inafuzu kushiriki michuano hii kwa mara ya nne ikiwa imefanya hivyo mwaka 1981, 2019, 2023 na sasa 2025. Kwa hatua hii Mheshimiwa Rais. Dkt. Samia Suluhu Hassan anaingia katika vitabu vya kumbukumbu na historia ya michezo nchini kwa kuwa Rais ambaye chini ya uongozi wake timu ya Taifa imefanikiwa kufuzu kushiriki mashindano haya makubwa zaidi kwa ngazi ya nchi barani Afrika mara mbili tena mfululizo. Mafanikio haya hayatokei kwa bahati mbaya na ni dhahiri kuwa ni matokeo uongozi thabiti na motisha kutoka kwa Rais Samia Suluhu Hassan. Sote tunafahamu namna ambavyo amekuwa akichochea timu za Taifa na hata vilabu vinavyoshiriki michuano ya kimataifa kupata matokeo chanya kwa kuweka motisha ya goli la Mama. Katika mchezo dhidi ya Ethiopia uliofanyika nchini Congo, Rais Samia alitoa ndege maalum iliyowapeleka wachezaji katika mchezo ule na kuwawezeshea kurejea kwa wakati nchini kujiandaa na mchezo dhidi ya Guinea ambao ndio umeipatia Tanzania tiketi ya kufuzu Afcon 2025. Ushindi dhidi ya Guinea ulichagizwa kwa kiasi kikubwa na nguvu ya mashabiki zaidi ya 60,000 walioujaza uwanja wa Taifa. Nakukumbusha tu mashabiki hawa wote waliingia bure kwani Rais Samia aliwalipia wote viingilio ili tu wajitokeze kwa wingi kuiunga mkono Taifa Stars. Habari njema zaidi ni kwamba baada ya Afcon 2025, michuano inayofuata mwaka 2027 Tanzania pia imo ndani kwani kwa mara ya kwanza michuano hii itafanyika katika ardhi ya Afrika Mashariki kwa ushirikiano wa Tanzania, Kenya na Uganda hivyo tayari tuna tiketi ya moja kwa moja. Mashindano haya kuja Afrika Mashariki… Read More
-
Kati ya mwezi Januari hadi Julai 2024 jumla ya ajira 607,475 zimezalishwa nchini ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali kufikia lengo la kuzalisha ajira milioni 1.2 kila mwaka. Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Patrobas Katambi ameeleza hayo bungeni jijini Dodoma. Jitihada za kuhakikisha watanzania wanapata ajira zinaakisi lengo la kuzalisha ajira milioni nane kama ilivyoelezwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) 2020-2025. Akizungumzia maeneo ambayo Serikali inayaangazia katika kuzalisha ajira ameeleza kuwa Serikali inatumia balozi zake kutafuta nafasi za kazi kwa watanzania kwenye maeneo yalipo balozi hizo. Vilevile ametaja njia nyingine kuwa ni kupitia taasisi za elimu, wizara na vyuo vikuu ambako baadhi ya watanzania wanapata ajira nje ya nchi, zikiwamo nafasi za utafiti na fursa kupitia mashirika ya Umoja wa Mataifa. Pia Naibu Waziri Katambi ameeleza kuwa Serikali tayari imeanza kutekeleza mpango maalumu kupitia Kitengo cha Huduma za Ajira Tanzania (TaESA) ili kubaini ajira zinazotangazwa mtandaoni na kuwafikia watanzania katika kanzidata, pia kuwasaidia kwa mafunzo ili kuhakikisha wanastahili kupata ajira hizo. Read More