#MiakaMitatuYaMama amezipatia majawabu changomoto za muda mrefu za watumishi wa umma

Watumishi wa umma wanayo mengi ya kufurahia na kuonesha katika miaka mitatu ya Mama kwani ametoa majawabu ya changamoto nyingi zilizokuwa za zinawakabili, hali iliyowaongezea motisha na ari ya kuwatumikia wananchi.

Kubwa la kwanza ambalo katika kila Sikukuu ya Wafanyakazi (Mei Mosi) lilikuwa likisubiriwa tangu mwaka 2016 ni nyongeza ya mishahara. Ndani ya uongozi wa Mama hilo limepatiwa majibu ambapo alipandisha kima cha chini cha mishahara kwa asilimia 23, nyongeza ambayo imewawezesha watumishi wa umma kumudu gharama za maisha ambapo pia aliahidi nyongeza itakuwa kila mwaka.

Kwa miaka saba, tangu mwaka 2016 watumishi hao hawakuwa wamepandishwa vyeo. Chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu watumishi 375,319 wamepandishwa vyeo ambapo Serikali imetumia TZS bilioni 85.89, fedha ambazo matumizi yake yamekwenda kuongeza mzunguko wa fedha na kuboresha maisha ya watumishi.

Ajira kilikuwa ni kilio kikubwa ambapo mbali na kuweka mazingira rafiki yaliyozalisha maelfu ya ajira kwenye sekta binafsi, Serikali tayari imeajiri watumishi wapya 81,137 katika taasisi mbalimbali za umma. Aidha, imetenga TZS bilioni 230 ambazo zitatumika kuajiri watumishi wapya 47,374 kabla ya mwaka wa fedha 2023/24 kumalizika.

Mama amekuwa akisisitiza kuwa yeye na wasaidizi wake si watawala bali ni watumishi wa wananchi. Ili kuhakikisha utumishi uliotukuka ameendelea kutatua changamoto zao ambao amewalipa malimbikizo maelfu ya watumishi. Ndani ya miaka mitatu ya Mama jumla ya watumishi 142,793 wamelipwa malimbikizo yenye thamani ya TZS bilioni 240.7.

Kwa lengo la kuendelea kuongeza ufanisi, Serikali imewabadilishia kada watumishi 30,924 ambapo imewalipa mishahara mipya yenye thamani ya TZS bilioni 2.56, mafanikio ambayo hayakuwa yamepatikana katika kipindi cha zaidi ya miaka mitano kabla ya uongozi wa Mama.

Kama hayo hayatoshi, kabla ya mwaka 2023/24 kumalizika, Serikali itakuwa imewapandisha vyeo watumishi 81,561 kwa gharama ya TZS bilioni 90.85, hatua hii mbali na kuongeza motisha kwa watumishi hao, utafungua fursa za ajira mpya.

Mbali na maslahi yao, Serikali imeboresha pia maeneo yao ya kazi ikiwemo kujenga majengo ya kisasa, mfano shule, hospitali, majengo ya utawala, kuwapatia vitendea kazi, ikiwemo magari na pikipiki pamoja na kujenga nyumba za watumishi ambazo pia zitapewa kipaumbele zaidi katika bajeti ya mwaka 2024/25.

Hata hivyo, kicheko hiki kipo pia kwa watumishi wa sekta binafsi ambapo kwa miaka tisa, tangu mwaka 2013 hawakuwa wamepata nyongeza ya mishahara hadi Serikali ya Awamu ya Sita ilipotangaza nyongeza ya mshahara wa kima cha chini Desemba 2022.