Ukuaji wa sekta za utalii, madini na viwanda waweka rekodi chini ya Mheshimiwa Rais Samia

Sera nzuri za uchumi za Mheshimiwa Rais Samia Suluhu zimeendelea kuweka rekodi ambazo hazijawahi kufikiwa katika historia ya taifa letu ambapo shughuli kuu za kiuchumi za utalii, madini na uzalishaji viwandani zimeendelea kufanya vizuri zaidi.

Mwaka 2023 mapato yatokanayo na utalii na dhahabu kwa mara ya kwanza yalivuka dola za Kimarekani bilioni 3 (zaidi ya TZS trilioni 7.6), huku uuzaji nje wa bidhaa za viwandani ukiendelea kuwa juu ya kiwango cha dola za Kimarekani bilioni 1 tangu MAMA aingie madarakani.

Matokeo haya ambayo hayakuwahi kufikiwa kabla ni ushahidi kuwa sera nzuri za Rais Samia zinalipa ambapo kupaa kwa mapato ya utalii na dhahabu kumeiwezesha nchini kupunguza urari wa biashara kutoka TZS trilioni 13.6 mwaka 2022 hadi kufikia TZS trilioni 7.2 mwaka 2023.

Takwimu toka Benki Kuu ya Tanzania zinaonesha kuwa shughuli mbalimbali za kiuchumi zimeimarika kuvuka kiwango kilichokuwepo kabla ya janga la UVIKO19, hali inayothibitisha kuwa, sio tu uchumi unaimarika kutoka kwenye janga hilo, bali unakuwa kwa kasi ambayo haijawahi kufikiwa kabla.

Wakati sekta za kiuchumi zikiendelea kufanya vizuri, mfumuko wa bei umeendelea kushuka ambapo kwa wastani mwaka 2023 ulikuwa asilimia 3 kutoka asilimia 3.2 mwaka 2022, sawa na malengo ya nchi na ukanda wa Afrika Mashariki na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika.