Serikali ya Mama ni Sikivu: Mikataba ya uwekezaji bandarini yajibu hoja za wananchi

Tanzania imefungua ukurasa mpya kwenye uwekazaji katika sekta ya uchukuzi kwa kusaini mikataba mitatu na kampuni ya DP World kwa ajili ya uwekezaji bandarini, uwekezaji ambao utashuhudia ufungwaji wa mifumo na mitambo ya kisasa itakayoleta mageuzi kwenye bandari, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuhakikisha inakuwa kitovu cha biashara na usafirishaji Afrika Mashariki na Kati.

Utiaji saini wa mikatanba mitatu ambayo ni mkataba wa nchi mwenyeji (HGA), mkataba wa uendeshaji gati namba 4 hadi 7 na mkataba wa ukodishaji gati namba 4 hadi 7 umetoa majibu kwenye hoja au maswali yaliyoibuliwa na wananchi yaliyotokana na mkataba wa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Dubai (IGA).

Moja ya hoja kubwa iliyoibuka wakati wa mjadala wa IGA ilikuwa ni ukomo wa mikataba, ambapo baadhi ya watoa hoja, hususani wanasiasa na wanaharakati walisema kuwa bandari hizo zimekabidhiwa kwa mwekezaji kwa muda usio na ukomo, wengine wakisema ni miaka 100. Hata hivyo, taarifa ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaa ya Bandari Tanzania imeeleza kuwa mikataba hiyo ni ya miaka 30, na kwamba mapitio ya utendaji wa mwekezaji yatafanyika kila baada ya miaka mitano kuona kama anatimiza vigezo alivyowekewa.

Pia, baadhi ya watoa hoja walidai kuwa Tanzania haiwezi kujitoa kwenye mikataba, lakini taarifa ya TPA imeeleza kuwa Serikali ya Tanzania inayohaki na inaweza kujitoa kwenye mikataba hiyo pindi itakapoona ni muhimu kufanya hivyo.

Aidha, mambo mengine yaliyoelezwa kutoka kwenye mikataba hiyo ambayo yanajibu maswali ya wananchi ni pamoja na sheria za Tanzania kutumika kwenye mikataba husika, serikali kuwa na umiliki wa hisa kwenye kampuni itakayoendesha sehemu ya bandari, mwekezaji kulipa kodi kwa mujibu wa sheria, masuala ya usalama kubaki kwa mamlaka za ndani, hakuna mtumishi wa bandari atakayepoteza kazi yake na kuwa uwekezaji huo utaihusu bandari ya Dar es Salaam.

Kwa upande wake Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amesema maoni ya watu wote yalizingatiwa katika kuandaa mikataba hiyo huku akiwatoa hofu Watanzania kwani maslahi ya Taifa yamepewa kipaumbele kwenye mikataba hiyo.

“Maboresho yanayokwenda kufanywa kupitia uwekezaji huu yatakuza biashara zetu za ndani na nje pamoja na kuwezesha shughuli za kiuchumi za nchi jirani. Hatua hii itaongeza mapato ya serikali na kuchangia kwenye uchumi wa taifa kwa ujumla, amesema Mheshimiwa Rais Samia.