Ziara ya Mheshimiwa Rais Samia nchini India itakavyofungua fursa kwa Tanzania

Mwaka 2022 Tanzania iliuza zaidi bidhaa zake nchini India, biashara ambayo ilichangia asilimia 17.3 ya mauzo yote, huku India ikiwa ni nchi ya tatu ambayo Tanzania iliagiza bidhaa nyingi zaidi (asilimia 12.5), takwimu ambazo zinadhihirisha namna mataifa haya yanauhusiano wa kibiashara wenye manufaa kwa pande zote.

Katika muktadha wa kukuza zaidi biashara na ushirikiano katika sekta nyingine, Rais wa Tanzania, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kufanya ziara ya kimkakati ya kitaifa ya siku tatu nchini India (Oktoba 8-10, 2023) kwa mwaliko wa Serikali ya India, ziara ambayo inatarajiwa kuwa matokeo chanya kwa Tanzania hasa katika sekta za afya, diplomasia, elimu, biashara na uwekezaji, uchumi wa bluu, maji, kilimo na teknolojia.

Ziara hiyo ni kubwa kwani inafanyika miaka na tangu kiongozi wa mwisho wa Tanzania kutembelea nchi hiyo, na inatarajiwa kuimarisha ushirikiano wa miaka 62 wa nchi hizo, ambao chimbuko lake ni Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere na Waziri Mkuu wa India, Hayati Jawaharlal Nehru.

Ziara ya Mheshimiwa Rais nchini India ina malengo makubwa mawili ambayo ni kudumisha, kuimarisha na kuendelea uhusiano uliopo katika sekta takribani 10 na kufungua fursa za biashara na uwekezaji, ikifahamika kuwa India ni moja ya nchi zenye uchumi mkubwa duniani na ni moja yenye miradi mingi ya uwekezaji nchini.

Matarajio ya mafanikio kutokana na ziara hiyo;

ELIMU
1. Fursa za mafunzo kwa Watanzania katika nyanja mbalimbali nchini India ambapo kwa kuanzia kutatolewa nafasi 1,000.

BIASHARA VYA UWEKEZAJI
1. Kuongezeka kwa uwekezaji nchini hasa viwanda vya kutengeneza simu na vifaa vya kielektroniki

AFYA
1. Kuanzishwa kwa taasisi ya upandikizaji wa figo hapa nchini

2. Kuanzishwa kwa kiwanda cha kutengeneza chanjo za binadamu na wanyama

3. Kuongeza ushirikiano kati ya hospitali za Tanzania na India ili kuimarisha uwezo na weledi katika utoaji wa huduma za afya.

4. Kuongezeka kwa upatikanaji wa dawa (ubora na unafuu)

KILIMO
1. Kufungua fursa zaidi za masoko ya mazao ya kilimo, ambapo matokeo yameanza kuonekana kwani kupanda kwa bei ya mbaazi kumetokana na India kuongeza ununuaji.

2. Kuvutia uwekezaji kwenye kilimo na mnyororo wa thamani ikiwemo kuanzisha kongani ya viwanda katika eneo la ekari 1,000.

UCHUMI WA BLUU
1. Kuanzishwa kwa karakana ya utengenezaji wa vyombo vya majini kutokana na uwepo wa bahari, maziwa na mito

MAJI
1. Kuingia hatua ya pili ya mradi wa kutoka maji Ziwa Victoria pamoja na mradi wa kufikisha maji katika miji 28

Ili kufanikisha malengo haya yote, akiwa nchini India, Mheshimiwa Rais Samia ambaye ataambatana na viongozi wa serikali, wafanyabiashara na viongozi wa sekta binafsi atakutana na kufanya mazungumzo na wafanyabiashara mbalimbali wa India katika kutangaza fursa za ushirikiano, biashara na uwekezaji.