Mheshimiwa Rais Samia apongezwa kila kona kwa kuongeza ‘boom’ vyuo vikuu

Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ameridhia ombi la wanafunzi wa elimu ya juu nchini kwa kuongeza fedha za kujikimu kutoka TZS 8,500 HADI TZS 10,000, kauli ambayo iliibua shangwe huku wanafunzi wakiimbia “tuna imani na Samia,” pamoja na kupiga makofi ya furaha.

Wakati wanafunzi hao wakishangilia kwa aamuzi huo uliokonga nyoyo zao, Rais Samia amesema ombi lao la wanafunzi wa ngazi ya stashahada na astashahada kupatiwa mikopo litawekewa mipango kwanza.

“Kwa kazi tunazozifanya sasa hivi na hali ya bajeti, hili bado hatujafikia huko, kwa hiyo tunalifikiria, tunaliweka kwenye mipango yetu,” amesema Rais Samia huku akieleza amemuagiza waziri wa fedha aangalie uwezekano wa kupata fedha, akifanikiwa atamuongezea nyingine ili wananchi hao wanufaike.

Wakati hayo yakiendelea, Rais Samia ameeleza mikakati ambayo Serikali yake inachukua kuwawezesha wahitimu kujiajiri pindi wanapohitimu masomo yao ikiwa ni pamoja na mapitio ya mitaala na kuhimiza elimu na matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.

“Tunataka elimu isiwe chanzo cha changamoto ya ajira, bali itoe suluhisho […] Ndio maana tumejielekeza sana sasa kwenye elimu ya TEHAMA ili vijana muweze kujiajiri wenyewe,” amesema Rais Samia.

Wanafunzi wa elimu ya juu wakiwakilishwa na viongozi wao wamemshukuru Rais Samia kwa hatua ambazo ameendelea kuchukua kuboresha elimu ya juu nchini ambapo wameanza kuona matokeo.