Historia imeandikwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia akizindua ujazaji maji Bwawa la Nyerere

Safari ya miaka 50 ya kuelekea umeme wa kutosha leo imepiga hatua kubwa baada ya Bwawa la Kufua Umeme wa Maji la Julius Nyerere (JNHPP) kuanza kujazwa maji leo zoezi ambalo limezinduliwa la Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan baada ya kufunga mahandaki yaliyokuwa yakichepusha maji ili kupisha ujenzi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt. Samia amesema kuwa mradi huu ambao ujenzi wake ulianza mwaka 2018 ni mojawapo ya miradi mikubwa ya umeme barani Afrika ambapo bwawa hilo litaweza kuhifadhi maji lita bilioni 32, hivyo kuwezesha shughuli za umeme kuendelea pindi mvua zinapopungua.

Dkt. Samia amekuwa na mchango mkubwa katika mradi huo ambao utaleta manufaa ya kiuchumi na kijamii, ambapo ndani ya miezi 22 amefanikiwa kujenga asilimia 41.68 ya mradi huo, wakati hapo awali ulijengwa asilimia 37 kwa muda wa miezi 27.

Akitaja manufaa mengine ya mradi huo mbali na umeme utakaokizi mahitaji ya ndani na hata kuuzwa nje, amesema kuwa utachochea ukuaji wa sekta ya utalii, kutokana na kuwa katika Hifadhi ya Taifa ya Nyerere, na pia kuwezesha fursa za uvuvi, ambapo bwawa hilo lenye urefu wa kilomita 100 litakapojaa litakuwa na ukubwa kuliko Ziwa Rukwa, hivyo ametaka ufanyike uvuvi wa kisasa.

Kuhusu kilimo, amesema mradi huo utafungua fursa za kilimo katika Delta ya Rufiji na hivyo ameiagiza wizara ya kilimo, wizara ya ardhi na TAMISEMI kupima eneo la ekari 400,000 linalofaa kwa kilimo na kufanya mnada wa wazi kwa wawekezaji wa uhakika katika kilimo.

“Nawasihi pia, tutenge maeneo maalum kwa ajili ya wakulima wadogo wadogo, hasa wa maeneo haya, yatakayokuwa na miundombinu ya umwagiliaji,” ameagiza.

Aidha, katika mradi huo limejengwa daraja la kudumu ambalo linaiunganisha mikoa ya kusini na mikoa ya kati na kaskazini mwa Tanzania, ambapo msafiri ataweza kutoka Mtwara kwenda Dodoma, Arusha au Kilimanjaro bila kupita Dar es Salaam. Pia, kutokana na bwawa hilo kuwa na maji mengi, ameagiza DAWASA kuona namna ya kutumia maji hayo kwa ajili ya matumizi kwa mkoa wa Dar es Salaam.

Zoezi la ujazaji maji katika bwawa hilo litakamilika mwaka 2024, na hivyo kuruhusu zoezi uzalishaji umeme kuanza Juni 2024, hatua ambayo italeta mageuzi ya kiuchumi kwa kuvutia wawekezaji kutokana na kuwepo umeme wa uhakika na gharama nafuu.