Miaka 61 ya Uhuru: Rais Dkt. Samia anavyotumia misingi ya Mwl. Nyerere kuchochea maendeleo

Tanzania Bara leo imeadhimisha miaka 61 tangu ipate Uhuru kutoka kwa Uingereza mwaka 1961, safari ambayo Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema “imekuwa safari yenye changamoto na mafanikio mengi ambayo Taifa letu linajivunia.”

Katika kuadhimisha siku hii kubwa, mjadala mkubwa huzunguka mchango wa Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika Uhuru, na misimamo aliyoiweka ambayo imekuwa ikitumiwa kama rejea katika kuliongoza Taifa. Mambo mengi ambayo aliyahimiza, Rais Samia ameendelea kuyahimiza na kuyatekeleza ili kuchochea maendeleo ya Watanzania ambayo ni pamoja na;

1. Kupiga vita rushwa
Mwalimu Nyerere alikiri kuwa, katika awamu ya kwanza kulikuwa na rushwa, lakini walikuwa wakali sana kuipinga. Serikali yake ilipitisha sheria, mtu akithibitika amepokea au ametoa rushwa, atahukumiwa kifungo kisichopungua miaka miwili na viboko 24 (12 akiingia na 12 akitoka).

Vivyo hivyo, Dkt. Samia ameendeleza ari hiyo ya kupinga rushwa akiamini kuwa rushwa inaathiri utoaji haki kwa kumwacha mwenye hatia mtaani na kumfunga asiye na hatia, inawanyima wasio na uwezo fursa ya kupata huduma lakini pia ni kinyume na mafundisho wa kidini.

2. Huduma za Jamii (Elimu, Maji na Afya)
Mara baada ya Uhuru, Mwalimu Nyerere aliainisha maadui watatu wa Taifa ambao ambao ni Ujinga, Maradhi na Umasikini. Katika miaka miwili ya Dkt. Rais madarakani amejipambanua kwa kupamba na maadui hao ambapo amewezesha ujenzi wa madarasa zaidi ya 23,000, shule mpya, ajira za walimu, vituo vya afya zaidi ya 230, kujenga na kukarabati hospitali, kufufua na kuanzisha na kukamilisha miradi ya maji pamoja na kuajiri watumishi katika sekta hizo ili kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.

3. Kilimo cha kisasa
“Tubadili kilimo chetu kusudi kilimo kitusukume kwa sababu hatuna kitu kingine cha kuisukuma nchi hii isipokuwa ni kilimo. Lakini kilimo hiki cha jembe la mkono, kilimo hiki cha kutegemea mvua peke yake, hakina mbolea, hakina dawa, unapanda hovyo hovyo tu, hakitusaidii sana,” alisema Hayati Mwalimu Nyerere.

Kwa upande wake, Rais Samia amefanya mageuzi kwanza kwa kuongeza bajeti ya kilimo kwa zaidi ya asilimia 200, ameanzisha mashamba makubwa ya umwagiliaji, ametoa vitendea kazi na elimu kwa maafisa ugani, ametoa TZS bilioni 150 ya ruzuku ya mbolea, ametoa pembejeo za kilimo bure kwa wakulima na kufungua masoko ya bidhaa nje ya nchi, ili kuhakikisha wakulima wananufaika na kilimo kinachingia ukuaji wa uchumi.

4. Kupinga Ukabila
Kama ambavyo Mwalimu Nyerere alivyosisitiza kuwa mtu hatochaguliwa au hatoacha kuchaguliwa kwa sababu ya kabila lake, Rais Samia ameendelea kusisitiza kuwa katika Serikali anayoiongoza hatamteua au kumwajibisha mtu kutokana na kabila lake, bali itafanya hivyo kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za nchi.

Pia amewaonya viongozi na wote wanaopigia chapuo ukabila, huku akiwataka wananchi kuendelea kujitambulisha kama Watanzania ili kujenga umoja ambao ni nguzo ya maendeleo.

5. Demokrasia na haki
Kwa takribani miaka miwili ambayo ameiongoza Tanzania, Rais Samia amefanikiwa kuimarisha demokrasia, uhuru na haki za wananchi nchini, ikiwa ni masuala ambayo Mwalimu Nyerere alikuwa akiyahimiza na kusema kwamba hayana mbadala.

Mwalimu Nyerere alisema katika mijadala waliyokuwa nayo haikuwa ikijadili kama demokrasia ni muhimu au sio muhimu bali ilijikita katika kuangalia namna gani ya kuitekeleza demokrasia. Aidha, alisema nchi haiwezi kusema kuwa ina maendelea ikiwa watu wake wana hofu juu ya usalama wao, jambo ambalo Rais Samia amefanikiwa kuimarisha usalama na haki ikiwa ni pamoja na kuagiza waliobambikiwa kesi waachiwe na kukomesha matumizi ya nguvu katika sehemu zisizotakiwa.

Katika siku hii muhimu, Rais Samia amewasihi Watanzania kutumia “siku hii kutafakari na kuweka dhamira ya kuongeza juhudi na maarifa ya kulipeleka Taifa letu mbele na kwa kasi zaidi.”