Rais Samia aja na suluhu kukamilisha mradi wa maji Same – Mwanga – Korogwe baada ya kukwama kwa zaidi ya miaka 10

“Katika miradi mirefu, ya siku nyingi, inatengenezwa na kusita, na kusimama, ni Same – Mwanga. Tutakwenda kutafuta fedha tuhakikishe unatekelezwa na mwakani […] wapate maji.”

Ni maneno ya matumani aliyoyatoa Rais Samia Suluhu Hassan Juni 2022 akiuelezea mradi wa maji wa Same – Mwanga – Korogwe ambao ulikwama kwa zaidi ya miaka 10, na kuyeyusha matumaini ya wananchi zaidi ya nusu milioni kupata maji safi, salama na ya uhakika.

Alipoingia madarakani Machi 2021, Rais alikuta mradi huo wa bilioni 262 wenye uwezo wa kuzalisha maji lita milioni 65 kutoka katika Bwawa la Nyumba ya Mungu ukikabiliwa na changamoto za kisheria na kifedha, akafanikisha kutatuliwa kwa changamoto za kisheria na kuingiza TZS bilioni 36 ili mradi ukamilike wananchi wapate maji safi na salama.

Kwa sasa, wakazi wa maeneno hayo wana matumaini ya kupata maji mapema mwaka 2023 ambapo hadi Aprili 2022 utekelezaji ulikuwa umefikia asilimia 70.4.

Kutokana na changamoto za kisheria, Serikali ilivunja mkataba na wakandarasi M.A Kharafi & Sons na kampuni ya Badr East Africa Enterprises kwa makosa ya kugushi nyaraka muhimu za kimkataba pamoja na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu, kisha mradi huo ukakabidhiwa kwa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA).