Rais amesikia, ametekeleza: Watumishi 14,500 walioondolewa kwa vyeti feki kurejeshewa mafao yao

Rais Samia Suluhu Hassan ameutafsiri kwa vitendo msemo ‘Haki haipaswi tu kutendeka, ni lazima ionekane inatendeka,’ baada ya kuridhia kurejeshwa michango ya watumishi 14,516 waliobainika kuwa na vyeti vya kughushi na waliondolewa kwenye utumishi wa umma.

Ridhaa hiyo ya Rais inamaanisha kuwa Serikali itatoa TZS bilioni 46.8 ambazo zitarejeshwa kwa watumishi hao walioondolewa kazini kati ya mwaka 2016 na 2017 katika zoezi la uhakiki wa watumishi wa umma.

Fedha hizo ni makato ya asilimia 5 ambayo watumishi hao walikatwa kwa muda waliofanya kazi. Kurejeshwa kwa fedha hizo kunadhihirisha azma ya Rais Samia kuona haki ikitendeka kwa Watanzania wote na kwa wakati wote.

Ikiwa ni miaka 5 imepita tangu watumishi hao walipoondolewa kwenye utumishi wa umma, kwa muda wote wamekuwa wakiiomba Serikali kufanya hivyo, huku wabunge na vyama vya wafanyakazi pia vikishinikiza hilo, hivyo uamuzi wa kutekeleza ombi hilo kunaonesha namna Rais alivyomsikivu na anayafanyia kazi maoni na mapendekezo ya Watanzania.

Wanufaika wote hao ambao waliondolewa kazini bila kujiandaa hivyo kukumbana na changamoto mbalimbali za kimaisha, sasa wataweza kutumia fedha hizo kuboresha maisha yaona kujiendeleza kiuchumi.

Baadhi ya waliohojiwa na vyombo vya habari wamesema kwamba hawaamini hilo limefanyika huku wakielekeza shukrani zao kwa Rais Samia kwa kuwezesha jambo hilo ambalo lilikwama kwa muda mrefu, na kwamba tayari walikuwa wamekata tamaa kuwa hatitofanyika tena.