Historia, Rais Samia akizima majenereta na kuwasha umeme wa gridi ya Taifa Kigoma

Rais Samia Suluhu Hassan leo Oktoba 17, 2022 kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi amewasha umeme wa Gridi ya Taifa katika Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma na kuzima mitambo mitatu ya mafuta yenye iliyokuwa ikizalisha umeme megawati 3.75 zilizotumika Wilaya ya Kasulu na Buhigwe.

Uzimaji wa majenereta wilayani Kasulu ni mwendelezo wa uzimaji majenerata katika maeneo mbalimbali baada ya umeme wa gridi ya Taifa, ambapo maeneo mengine ni Kibondo, Loliondo, Ngara na Biharamulo.

Kwa kuendesha majenereta kwa mkoa wa Kigoma pekee, Serikali ilikuwa ikipata hasara ya TZS bilioni 36 kila mwaka, kwani gharama za uendeshaji majenereta ilikuwa TZS bilioni 52 huku mapato yakiwa TZS bilioni 14.

Mbali na kuondoa hasara hiyo umeme wa gridi ya Taifa utawezesha wakazi wa Kigoma kupata umeme wa kutosha ambapo uhitaji ni megawati 14, na Serikali imepeka megawati 20.

Aidha, umeme utachochea shughuli za kiuchumi na uwekezaji katika sekta za biashara, viwanda, madini na kilimo, hivyo kuongeza mapato ya wananchi na Taifa. Pia, umeme utaimarisha shughuli za ulinzi na usalama na utoaji huduma zakijamii kwa wananchi na kuchochea ukuaji wa sekta nyingine.